Na Lucy Ngowi
DODOMA: WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amelielekeza Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kuharakisha matumizi ya teknolojia za kisasa, kujitegemea kifedha na kuongeza utoaji wa elimu kwa umma ili kuimarisha ubora wa bidhaa, kurahisisha biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Kapinga ametoa maelekezo hayo wakati wa kilele cha maadhimisho ya miaka 50 ya TBS, akisema shirika hilo lina nafasi muhimu katika kufanikisha azma ya Tanzania ya kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani katika soko la ndani na kimataifa.
Amesema baada ya kufikisha miaka 50, TBS inapaswa kuanza kujitegemea zaidi kifedha badala ya kuendelea kutegemea ruzuku kutoka Serikalini.

“Miaka 50 ni umri wa taasisi iliyokomaa. Ni wakati wa TBS kujitegemea na kuondoa mzigo kwa mfuko mkuu wa Serikali huku ikichangia zaidi maendeleo ya taifa,” amesema.
Waziri huyo pia amesisitiza umuhimu wa kuboresha mifumo ya kidijitali na kuunganisha huduma za TBS na taasisi nyingine ili kupunguza vikwazo vya biashara, hususan katika maeneo ya mipakani.
Amesema dunia imebadilika na kwamba wananchi wanapaswa kuwa na uwezo wa kuthibitisha ubora wa bidhaa kwa kutumia teknolojia za kisasa kama mifumo ya kielektroniki inayoweza kusomwa kwa njia ya simu.
Kapinga ameongeza kuwa TBS ina jukumu kubwa la kulinda afya ya jamii kupitia udhibiti wa ubora wa vyakula na vipodozi, hivyo ni muhimu kuanzisha programu endelevu za kutoa elimu kwa wananchi kuhusu viwango vinavyotakiwa kufuatwa katika bidhaa mbalimbali.
Aidha, amewataka watendaji wa shirika hilo kujiona kama wawezeshaji wa biashara na viwanda badala ya kuwa kikwazo kwa wawekezaji na wafanyabiashara.
Akizungumzia mafanikio ya TBS katika kipindi cha miaka 50, Kapinga amesema yamechangiwa na maono ya viongozi waliopita, juhudi za wafanyakazi pamoja na ushirikiano wa wadau mbalimbali.
Ameeleza matarajio ya Serikali kuwa katika miaka 50 ijayo, TBS itaendelea kuwa taasisi ya kisasa, bunifu na yenye uwezo mkubwa wa kukabiliana na mabadiliko ya teknolojia, biashara na mahitaji ya soko la dunia.

