Na Lucy Lyatuu, Dodoma
SHIRIKA la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) linasisitiza umuhimu wa kutumia dawa kwa ajili ya mifugo pale inapobidi na kwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu au chini ya uangalizi wa wataalamu wa afya ya mifugo.
Ujumbe huo umetolewa na Mratibu Wa Miradi Ya Udhibiti Wa Usugu Wa Vimelea Vya Magonjwa Dhidi Ya Dawa kutoka FAO, Elibariki Mwakapeje, wakati akizungumza katila maonesho ya Nanenane yanayoendelea Dodoma.

Amesema elimu hiyo inalenga kuwajengea wafugaji uelewa kuhusu matumizi sahihi na yenye uwajibikaji ya dawa za mifugo, pamoja na madhara yanayoweza kujitokeza endapo dawa zitatumika bila kuzingatia ushauri wa wataalamu.
Amesema wanatumia Maonesho ya Nane Nane kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu namna ya kukabiliana na usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa, hali inayoweza kupunguza ufanisi wa dawa za kutibu na kudhibiti magonjwa kwa mifugo.
Mwakapeje amesema wafugaji wanapaswa kuepuka kutibu mifugo bila ushauri wa wataalamu wa afya ya mifugo, huku akisisitiza umuhimu wa kutumia dawa pale inapobidi na kwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu au chini ya uangalizi wa wataalamu wa afya ya mifugo.

Ameongeza kuwa wafugaji wanapaswa pia kuzingatia usafi wa mazingira, mabanda, vyombo vya maji na chakula cha mifugo, hatua inayosaidia kuzuia na kupunguza maambukizi ya magonjwa na hivyo kupunguza utegemezi usio wa lazima wa dawa katika kutibu mifugo.
Kwa mujibu wa Mwakapeje, matumizi holela ya dawa yanaweza kuongeza usugu wa vimelea vya magonjwa, jambo linaloweza kuathiri afya ya mifugo, wanyama wengine, binadamu na usalama wa chakula.
Amesema suala hilo linahitaji ushirikiano wa wafugaji, wataalamu wa afya ya mifugo na wadau wengine katika mnyororo wa chakula ili kuhakikisha dawa zinatumika kwa usahihi.
Amesema FAO itaendelea kutumia majukwaa kama Maonesho ya Nane Nane kuwaelimisha wananchi kuhusu matumizi salama na yenye uwajibikaji ya dawa, akisisitiza ujumbe wa “Kinga ni bora kuliko tiba” katika mapambano dhidi ya usugu wa vimelea vya magonjwa na kulinda afya ya mifugo pamoja na usalama wa chakula.

