Na Lucy Ngowi
DODOMA: JESHI la Magereza limewataka wananchi kubadili mtazamo dhidi ya wafungwa wanaomaliza vifungo vyao kwa kuwapa fursa ya kuanza maisha mapya, likieleza kuwa mfumo wa kisasa wa magereza unalenga zaidi marekebisho ya tabia na kuwaandaa wahusika kuwa raia wema baada ya kutumikia adhabu zao.
Akizungumza katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, Kamishna Msaidizi wa Jeshi la Magereza, Elmas Mgimwa, amesema taasisi hiyo imeimarisha programu za marekebisho zinazowajengea wafungwa ujuzi na stadi mbalimbali za maisha ili waweze kujitegemea wanaporejea katika jamii.

Amesema mbali na jukumu la msingi la kupokea na kuhifadhi wafungwa kwa mujibu wa sheria, magereza yanaendesha mafunzo ya ufundi stadi, kilimo, ujasiriamali na elimu nyingine zinazowawezesha wafungwa kupata maarifa yatakayowasaidia kujenga maisha yao baada ya kifungo.
“Tunataka kila anayemaliza kifungo atoke akiwa amepata mabadiliko chanya, maarifa na ujuzi wa kujitegemea ili aweze kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya familia yake na taifa kwa ujumla,” amesema Mgimwa.
Amefafanua kuwa mchakato wa marekebisho huanza tangu mfungwa anapopokelewa gerezani, kupitia programu za kujenga maadili na tabia njema, hadi hatua ya kuandaliwa kurejea katika jamii.

Mgimwa amesisitiza umuhimu wa wananchi kuwaunga mkono waliomaliza vifungo badala ya kuwabagua, akieleza kuwa lengo la kifungo ni kutoa nafasi ya marekebisho kama ambavyo mgonjwa hupatiwa matibabu ili kurejea katika hali bora.
Aidha, amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea na maandalizi ya kuanzisha mfuko maalumu utakaowawezesha wafungwa wanaomaliza vifungo kuanzisha shughuli za kiuchumi kulingana na stadi walizopata wakiwa magerezani.
Kwa mujibu wa Mgimwa, hatua hiyo itachangia kupunguza matukio ya wahusika kurejea katika makosa ya jinai na badala yake kuwa sehemu ya nguvu kazi inayochochea maendeleo ya nchi.Pia, Jeshi la Magereza linaendelea kufuatilia maendeleo ya waliomaliza vifungo ili kuhakikisha wanatumia vyema elimu na ujuzi walioupata wakati wa kutumikia adhabu zao.

