Na Lucy Lyatuu,Dodoma
SHIRIKA La Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC) limesema lina mpango wa kusogeza huduma ya vituo vya kusambaza gesi nchi nzima na kwamba ndani ya miaka miwili na nusu kuanzia sasa huduma hiyo itafikishwa.
Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kutangaza miradi ya maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/2026.
Amesema TPDC inahimiza ujio wa vijana kwenye sekta ya nishati, ambapo asilimia 79 ya wafanyakazi ni vijana.
Kuhusu kusogeza huduma ya vituo vya CMF amesema kwa sasa Tanzania Ina vituo 14 peke yake na vimejengwa katika mkoa wa Dar es Salaam na Kwa kuanzia huduma hiyo itasogezwa katika vituo vidogo katika mkoa ya Tanga,Kilimanjaro,Arusha, Dodoma na Morogoro ambapo vitafikisha gesi kama ilivyo bila kuchakatwa.
Amesema kwa maneno mengine Kwa kushirikiana na kampuni mbalimbali gesi itafikishwa kwa mfumo wa LNG yaaani kubadilisha gesi kuwa kimiminika ambapo itafikishwa nchi nzima ndani ya kipindi hicho.
Aidha amesema nyumba 2500 kutoka mikoa ya Mtwara,Lindi na Dar es Salaam zitaunganishwa Kwa gesi.
Ameongeza kuwa TPDC inaendelea kuchangia maendeleo ya Taifa kwa kuendesha miradi mikubwa ya nishati, huku ikiweka kipaumbele katika kuwajengea uwezo vijana wa Kitanzania.
Almesema katika mwaka wa fedha 2025/2026, TPDC inaendelea kutekeleza miradi kwa Awamu , inayolenga kuongeza upatikanaji wa gesi asilia, kupanua usambazaji wa mafuta na gesi, na kutoa fursa kwa vijana kuajiriwa, kupata mafunzo na kushiriki katika mnyororo wa thamani wa sekta ya nishati.
Amesema Serikali ipo katika hatua za mwisho za majadiliano ya mradi wa gesi asilia wa kimkakati unaogharimu Dola bilioni 42 na kwamba TPDC inahakikisha ushiriki wa vijana na wazawa katika ajira, ujenzi, zabuni, huduma za kitaalamu, TEHAMA, na malazi.
Ameitaja miradi mikuu inayotekelezwa na Shirika hilo ni pamoja na Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), ambapo ujenzi wa bomba kutoka Hoima, Uganda hadi Bandari ya Tanga umefikia asilimia 81 na unatarajiwa kukamilika Julai mwaka huu na kwamba mradi huo unatoa ajira,fursa za zabuni na uhamasishaji wa ujuzi kwa Watanzania.
“Fursa zinazotolewa ni ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja, mafunzo ya vitendo, zabuni, “internship programs” na uwezeshaji wa sekta za kiuchumi kama usafirishaji, viwanda na hoteli,” amesema.
Kuhusu miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), ameeleza kuwa
zaidi ya Sh bilioni 11.5 zimegawanywa kwenye miradi ya kijamii ikiwemo ujenzi wa vituo vya afya, shule, kivuko, taa za barabarani, na kituo cha polisi.
Akizungumzia uchorongaji wa visima vitatu Mnazibay, Mtwara ameeleza kuwa Kisima cha kwanza (MB-5) kimeanza Februari mwaka huu na miradi yote itakamilika Oktoba 2026.
Makame Akizungumzia utafutaji wa mafuta Kitalu cha Eyasi Wembere amebainisha kuwa TPDC inaendelea na uchukuaji wa taarifa za 2D katika mikoa ya Singida, Tabora, Simiyu, Arusha na Shinyanga, ukikamilika Juni 2027 kwa gharama ya Shilingi bilioni 53.4.

