Na Lucy Lyatuu,Dodoma
MABORESHO yaliyofanywa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kupata huduma kupitia PSSSF Kidijitali yameleta urahisi kwa wanachama wa Mfuko hu.
Hayo yamebainishwa na wanachama wa Mfuko waliotembelea kwenye banda la PSSSF kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kwenye viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Ofisa Utumishi wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TARIRI), Odilia Marenga amebainisha alipotembelea banda la huduma la PSSSF katika viwanja hivyo kuwa watumishi wa TARIRI walionufaika na mafao kutoka PSSSF ni shuhuda, wamekuwa wakipiga simu kueleza furaha yao kwa jinsi walivyopokea mafao haraka.

“Tangu huduma zianze kutolewa kupitia PSSSF portal, zimekuwa zikitolewa kwa wakati, tofauti na hapo nyuma… hali hii imekuwa ikiwafurahisha wastaafu wetu na wale akina mama wanaoomba fao la uzazi,” amesema Marenga.
Kwa upande wake Mwanachama wabPSSSF Rebeca Hoza, amesifu huduma ya PSSSF Kidijitali, ambayo amekuwa akipata huduma kupitia kiganjani.
“Nikitaka kuangalia michango yangu au taarifa zozote, sihangaiki tena, PSSSF wamefanya maisha yetu kuwa rahisi.” amesema.
Kuhusu mafanikio ya utoaji huduma, Kaimu Meneja wa PSSSF Kanda ya Kati- Dodoma, Jane Mbuya amewashukuru wanachama wa PSSSF kwa kuonyesha ushirikiano kwa kutumia huduma hiyo ya PSSSF portal.

“Ushuhuda ni kwamba hata ukipita kwenye ofisi zetu hutakuta foleni za wanachama wakipata huduma, kwani tumesogeza huduma kupitia PSSSF Kidijitali hii imeturahisishia, sasa hivi tunachakata mafao ya mstaafu kabla hajaondoka ofisini, akistaafu na mafao yake yako tayari, hii ni kutokana na kutumia mifumo kutoa huduma,” amesisitiza Mbuya.


