Na Lucy Ngowi. Mwanza
OFISA Uhifadhi na Uvuvi kutoka taasisi ya Blue Victoria, Alice William, amesema tafiti zinaonyesha kuwa nyavu nyingi za uvuvi zinazotumika katika Ziwa Victoria hutengenezwa kwa plastiki, na zinapoendelea kukaa ndani ya maji hupasuka na kutoa chembechembe ndogo zinazoliwa na samaki, hali inayoweza kuhatarisha afya za binadamu.
Alice amesema samaki wanapomeza chembechembe hizo za plastiki hubaki kwenye misuli yao, na baadaye mlaji wa mwisho ambaye ni binadamu hupata madhara mbalimbali kiafya.
“Nyavu hizi zinapooza au kupukutika ndani ya maji, hutoa chembechembe za plastiki ambazo samaki huzila. Mwisho wa siku binadamu ndiye anayebeba athari hizo kupitia ulaji wa samaki,” amesema Alice.
Ameeleza kuwa Blue Victoria ni taasisi isiyo ya kiserikali inayojihusisha na uhifadhi wa bayonuai zilizopo ndani ya Ziwa Victoria, huku shughuli zake zikifanyika katika maeneo ya bonde la ziwa, ikiwemo Mkoa wa Mwanza.
Mbali na uhifadhi wa mazingira, taasisi hiyo pia imekuwa ikiwawezesha wanawake na vijana kuongeza kipato kupitia shughuli za kuongeza thamani ya zao la dagaa.
Amesema wamefanikiwa kujenga vichanja vya kukaushia dagaa katika Kisiwa cha Lukuba pamoja na eneo la Mwalo wa Mswahili jijini Mwanza.
Aidha, amesema taasisi hiyo imeanzisha matumizi ya teknolojia ya kisasa ya sensa (sensor) kwa ajili ya kukusanya taarifa za mazingira ya maji ili kusaidia kutatua tatizo la “kiferesi”, hali ya asili inayotokea ndani ya ziwa kutokana na kupungua kwa kiwango cha oksijeni kwenye tabaka la chini la maji.
Amesema tatizo hilo husababisha samaki aina ya sangara na sato kufa na kuelea juu ya maji, jambo linaloathiri shughuli za uvuvi na uchumi wa wananchi wanaotegemea ziwa hilo.
“Tunatumia sensa kupima hali ya maji mapema kupitia vipimo vya ubora wa maji (water parameters), ili wafugaji na wavuvi waweze kupata tahadhari kabla madhara hayajatokea,” amesema.
Kwa mujibu wa ripoti ya utekelezaji wa miradi ya mwaka 2025, Blue Victoria imefanikiwa kutoa elimu kwa jamii kuhusu madhara ya nyavu zilizotupwa au kutelekezwa ndani ya ziwa, maarufu kama “ghost nets”.
Ripoti hiyo imeeleza kuwa watu wengi wamekuwa wakiondoa taka ngumu kama plastiki na makopo lakini huacha nyavu za uvuvi majini bila kujua madhara yake kwa mazingira na afya ya binadamu.
Alice amesema hakuna kiwango salama cha plastiki kinachotakiwa kuwepo katika mwili wa binadamu, huku akionya kuwa hali hiyo inaweza kuchangia magonjwa mbalimbali ikiwemo saratani.
Kutokana na hali hiyo, taasisi hiyo imeendesha kampeni maalumu za kuondoa nyavu za uvuvi zilizotelekezwa ndani ya Ziwa Victoria ili kupunguza uchafuzi wa mazingira na kulinda afya za wananchi.

