Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Dennis Simba, amesema matumizi ya Mfumo wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST) yameleta mageuzi makubwa katika sekta ya ununuzi wa umma nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari Dodoma, Simba amesema mfumo huo umewezesha Serikali kuongeza ufanisi katika michakato ya ununuzi, kupunguza muda wa kushughulikia zabuni pamoja na kuongeza uwazi na usawa kwa wazabuni.
Amesema takribani asilimia 70 ya bajeti yote ya Serikali hutumika kupitia ununuzi wa umma, hivyo mfumo huo unatoa fursa kwa wananchi, wajasiriamali na wazabuni kushiriki katika shughuli za Serikali kwa njia iliyo wazi na yenye ushindani.
“Mfumo wa NeST umekuja na mabadiliko makubwa katika sekta ya ununuzi wa umma, kwa kuongeza uwazi, ufanisi na kupunguza gharama za michakato ya ununuzi,” amesema Simba.
Ameeleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ilitoa msukumo wa matumizi ya teknolojia katika kuboresha usimamizi wa sekta ya ununuzi wa umma, hatua iliyowezesha NeST kuanza kutumika rasmi mwaka 2023.
Kwa mujibu wa Simba, kwa sasa mfumo huo una moduli sita ambazo ni usajili wa watumiaji (e-Registration), uendeshaji wa zabuni (e-Tendering), usimamizi wa mikataba (e-Contract Management), malipo (e-Payment), katalogia (e-Catalogue) pamoja na minada ya kielektroniki (e-Auction).
Amesema kupitia NeST, shughuli za ununuzi wa umma zinafanyika kwa njia ya kidijitali, jambo linalopunguza matumizi ya karatasi, gharama za usafiri na muda unaotumika katika michakato ya zabuni, huku pia likiongeza ufuatiliaji na uwajibikaji.
“Hatua hii imewezesha kuondoa kabisa uhusiano wa kuwa na nyaraka za kughushi kwenye mfumo, lakini pia kurahisisha mchakato wa kuwasilisha nyaraka husika wakati wa michakato ya zabuni,” amesema Simba.
Aidha, amesema PPRA inaendelea na hatua za kuunganisha NeST na mifumo mingine ya Serikali, ikiwemo mifumo ya malipo na benki, ili kuongeza ufanisi na kuhakikisha michakato ya ununuzi wa umma inakuwa salama, ya haraka na yenye uwazi zaidi.

