Na Lucy Lyatuu,Dodoma
MAMLAKA ya Udhibiti Wa Huduma Za Nishati Maji (EWURA) ,Idara ya umeme imesema katika mwaka wa fedha 2025/26 imetoa leseni zaidi ya 1002 Kwa mafundi umeme ambao wanastahili kufanya kazi hizo.
Aidha imewataka Wananchi kutumia mafundi umeme wanye leseni za Mamlaka hiyo,Ili kuepuka changamoto zitokanazo na hitilafu za umeme.
Mhandisi wa Mamlaka hiyo,Idara ya Umeme,Lulu Chilumba amesema hayo katika Banda la Mamlaka hiyo lililoko katika viwanja vya Bunge ikiwa ni kuadhimisha wiki ya Nishati 2026,wakati Katibu Mkuu Wizara Ya Nishati, (anayeshughulikia mafuta na Gesi) Dkt James Mataragio alipotembelea Banda hilo.

Amesema kupitia Shirika La Umeme Tanzania (TANESCO) mafundi hao wanaweza kupatikana na kusadia jamii kuepuka changamoto za hitilafu.
Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesema katika jitihada za kutatua changamoto zinazoikumba sekta ya nishati nchini, EWURA, imeelekeza nguvu zake Bungeni kwa kusogeza huduma, elimu na majibu ya moja kwa moja kwa wabunge wanaowakilisha wananchi.
Kupitia banda lake katika Wiki ya Nishati, EWURA inalenga si tu kutoa elimu, bali pia na kutatua hoja zinazotoka moja kwa moja kwenye maeneo ya wananchi.

“Hapa tunakutana na wabunge ambao ndio wawakilishi wa wananchi. Tunajibu maswali yao, lakini pia tunapokea maoni yatakayosaidia kuboresha huduma za nishati,” amesema.
Kuhusu Upatikanaji na Ubora wa Mafuta Ibrahim Kajugusi amesema EWURA ina jukumu la kuhakikisha mafuta yanapatikana kwa uhakika na kwa viwango vinavyokubalika.
Ameeleza kuwa mamlaka hiyo pia imerahisisha utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara ili kusogeza huduma hadi maeneo ya vijijini.
Kuhusu Gesi Asilia Mhandisi Evaline Rweikiza amesema matumizi ya gesi asilia yanaendelea kuongezeka, hasa katika magari na matumizi ya majumbani.
Amebainisha kuwa kwa sasa vituo 18 vya kujazia gesi vipo nchini, huku juhudi zikiendelea kupanua huduma hiyo nje ya Dar es Salaam ikiwemo Dodoma.
“Gesi asilia ni nafuu na inalinda mazingira, hivyo tunahamasisha matumizi yake kwa wananchi,” amesema.
Uwepo wa EWURA Bungeni umeonekana kuwa jibu la moja kwa moja kwa changamoto za nishati zinazowakabili wananchi, huku ukitoa nafasi kwa wabunge kuwasilisha kero za maeneo yao na kupata majibu ya papo kwa papo ambapo hatua hiyo inaashiria mwelekeo mpya wa uwajibikaji na ushirikishwaji katika kusimamia sekta nyeti ya nishati nchini.

