Na Lucy Ngowi
DODOMA:MFUKO wa Self Microfinance Fund (SELF) umeendelea kuhamasisha wananchi kutumia fursa za mikopo nafuu zinazotolewa na taasisi hiyo ili kukuza biashara, kuongeza uzalishaji na kuboresha hali ya maisha kupitia uwekezaji katika shughuli mbalimbali za kiuchumi.
Akizungumza katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, Meneja wa SELF Kanda ya Kati, Aristid Tesha, amesema mfuko huo umejikita katika kuwafikia wananchi wa makundi mbalimbali kwa huduma za kifedha zinazolenga kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Amesema SELF ina mtandao wa matawi 12 nchini unaohudumia Tanzania Bara na Zanzibar, huku Kanda ya Kati ikihudumia mikoa ya Dodoma na Singida.
“Tumejitokeza kwenye maonesho haya kutoa elimu kuhusu huduma za mikopo, ujasiriamali na usimamizi wa fedha. Wananchi wengi wamekuwa wakitembelea banda letu kupata taarifa na kufahamu namna wanavyoweza kunufaika na huduma tunazotoa,” amesema Tesha.
Kwa mujibu wa Tesha, SELF inatoa mikopo kwa watu binafsi wanaojishughulisha na shughuli halali za kiuchumi, pamoja na mikopo maalumu ya nishati safi inayowawezesha wafanyabiashara wa gesi, vifaa vya umeme na teknolojia za nishati ya jua kupata mitaji kwa masharti nafuu.
Aidha, mfuko huo hutoa mikopo ya jumla kwa vyama vya ushirika na taasisi ndogo za fedha zinazowakopesha wakulima, wafugaji na wananchi wa maeneo ya vijijini, hatua inayolenga kusogeza huduma za kifedha karibu zaidi na walengwa.
Ameongeza kuwa watumishi wa umma wanaweza kupata mikopo kupitia mfumo maalumu uliowekwa na mfuko huo, huku wananchi wengine wakinufaika na mikopo ya kuboresha makazi kwa ajili ya ukarabati au ukamilishaji wa nyumba zao.
Tesha amesema pia vikundi vya kijamii, SACCOS, wakulima na wafugaji wanaoshiriki katika minyororo ya thamani ya mazao na mifugo wana nafasi ya kupata mikopo inayowawezesha kuongeza uzalishaji na kuimarisha shughuli zao.
Mbali na huduma za mikopo, SELF pia hutoa huduma za bima za nyumba, vyombo vya moto na mali nyingine, sambamba na kutoa elimu ya bima kwa wananchi.
Ametoa wito kwa wananchi kutembelea banda la SELF kabla ya kuhitimishwa kwa maadhimisho hayo ili kupata elimu zaidi na kujionea fursa mbalimbali zinazotolewa na mfuko huo kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

