Na Mwandishi Wetu.
PWANI: MAMA Mchungaji wa Kanisa la Zinga Victory Tanzania Assemblies of God (TAG), lililoko Bagamoyo, Catherine Jovin amesheherekea siku yake ya kuzaliwa Juni Mosi, kwa kuungana na watoto Yatima na Mazingira Magumu katika Kituo cha Amani Orphanage Centre.

Akiwa kituoni hapo, Catherine amesema katika siku yake ya kuzaliwa ameona ni bora kuungana na watoto hayo ili kutoa kile Mungu alimchojalia, ambacho alifanya hivyo kwa kushirikiana na wanawake wa kanisa hilo.
Akizungumza na watoto hao, aliwataka wamtafute Mungu na kusoma kwa bidii,

“Ukiona huelewi darasani unasahau haraka vitu havieleweki, ni lazima iwepo bidii na umtafute Mungu kwa maombi.
” Soma pale shuleni, fanya home work kwa wakati. Zile kazi mnazopewa shuleni fanya kwa wakati, rudisha daftari kwa mwalimu usahishiwe ukikosea mwambie mwalimu kwa nini hapa nimekosea, onyesha bidii, hakuna nesi ambaye hajasoma, hakuna mwanajeshi ambaye hajasoma,” amesema hayo mama Mchungaji Catherine alipozungumzana watoto hao.

Amewaambia kwa kuwa kila mmoja anatamani kuwa fulani katika jamii, ni bora wasome kwa bidii kufikia ndoto zao, na kwamba wakimtumikia Mungu atawapa afya njema, atazidisha uzima ndani yao na kuwapa yote wanayoyahitaji,
Pia aliwakumbusha watoto hao kumpenda Mungu, aliwakumbusha kuwatii wazazi na kufanya yote wanayoelekezwa, ikiwa ni pamoja na kuishi maisha ya utakatifu.

Naye Happy Mitunu amewataka watoto hao wampende Mungu kwa kuwa atawafanikisha katika ndoto wanazotamani kuzifikia.

Kwa upande wake Meneja wa Kituo hicho chenye watoto 37, Decline Tirubuza alimshukuru Mama Mchungaji Catherine Jovin na ujumbe alioongozana nao kwa sadaka nzuri ya unga wa ugali, sukari na juisi waliyoikabidhi kwa kituo hicho kwa ajili ya kuhudumia watoto hao.

Amesema wakati wa masomo watoto 22 wanabakia kituoni hapo na wengine 15 wanakuwa shule za bweni hadi zitakapofungwa.
Amesema kituo hicho kinafanya kazi na Ustawi wa Jamii Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani, na ndio wanaopeleka watoto kituoni hapo.

