Na Lucy Ngowi
MWAKA 2022, ndani ya kundi la vijana wabunifu waliokusanyika kuwasilisha mawazo yao katika shindano la ubunifu lililoandaliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), kulikuwa na wazo moja lililolenga kutatua changamoto ambayo wakulima wengi wa Tanzania wamekuwa wakikabiliana nayo kwa miaka mingi,kupanda mbegu kwa gharama kubwa, kutumia nguvu nyingi na kupata tija ndogo.
Miaka minne baadaye, wazo hilo limegeuka kuwa Rafiki Planter, teknolojia rahisi ya kupandia mbegu inayobadilisha namna kilimo kinavyofanyika nchini.
Kwa wabunifu wake, mafanikio hayo ni ushahidi kuwa katika miaka 40 ya COSTECH, taasisi hiyo imeendelea kuibua vipaji, kulea ubunifu na kugeuza mawazo ya Watanzania kuwa suluhisho la maendeleo ya Taifa.
Ubunifu huo ulifanywa na watafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Kituo cha Ukiriguru mkoani Mwanza, wakiongozwa na Dauson Malela kwa kushirikiana na Dkt. Paul Saidia na Robert Cheleo.
Malela anasimulia kuwa hatua ya kwanza ilikuwa kutengeneza mashine ndogo yenye injini ya CC 125 na magurudumu ya chuma, wakiamini ndiyo yangekuwa bora zaidi kwa mazingira ya mashambani kuliko matairi ya mpira ambayo huweza kupata pancha kwa urahisi.
Hata hivyo, walipoipeleka mashine hiyo kwa wakulima kwa ajili ya majaribio, waligundua kuwa ubunifu hauishii maabara au karakana, bali hukamilishwa kupitia maoni ya watumiaji.

Tenkolojia iliyoboreshwa baada ya toleo la kwanza ambalo lilifadhiliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH)
“Wakulima walituambia wanahitaji mashine yenye injini yenye uwezo mkubwa zaidi na inayoweza kufanya kazi muda mrefu bila kupata joto. Pia walihitaji mashine iwe na magurudumu makubwa zaidi yanayofaa kwenye mazingira mbalimbali ya mashamba. Tulipokea maoni yao na kuanza maboresho,” anasema Malela.
Anasema hatua hiyo ndiyo iliyoifanya teknolojia hiyo ianze kuendana zaidi na mahitaji halisi ya wakulima.
Malela anaeleza kuwa maboresho hayo yasingewezekana bila msaada wa COSTECH, ambayo ndiyo taasisi ya kwanza kuamini wazo lao kupitia Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU).
“COSTECH ndiyo waliotushika mkono mwanzoni kabisa. Tulipoibuka washindi wa shindano la ubunifu mwaka 2022, walitupatia rasilimali za kuwezesha utengenezaji wa mashine imara, walituunganisha na wahandisi waliokuwa wakifanya kazi nasi bega kwa bega, na walitusaidia hadi hatua za usajili na ulinzi wa teknolojia yetu. Hapo ndipo safari ya mafanikio ya Rafiki Planter ilipoanza,” anasema.
Anasisitiza kuwa mchango wa COSTECH haukuishia kwenye fedha pekee, bali ulihusisha pia ushauri wa kitaalamu uliowawezesha kuboresha teknolojia yao kila walipokutana na changamoto mpya.

Toleo la kwanza chini ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia ( COSTECH), anayeendesha teknolojia hiyo ni Ofisa Mwandamizi wa COSTECH katika Mfuko wa Taifa wa Uendelezaji wa Sayansi na Teknolojia (MTUSATE), Ntufye Mwakigonja,
Baadaye, Wizara ya Kilimo kupitia Mradi wa Tanzania Food Systems Resilience Program (TFSRP) iliendeleza juhudi hizo kwa kuwezesha maboresho zaidi yaliyofanya Rafiki Planter kuwa teknolojia yenye uwezo mkubwa wa kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.
Leo, mashine hiyo inaweza kupanda ekari moja ndani ya dakika 45 hadi saa moja, kazi ambayo kwa kutumia jembe la mkono inaweza kuchukua zaidi ya saa nane na kuhitaji watu wengi.
Mbali na kuokoa muda na nguvu kazi, Rafiki Planter hupanda mbegu kwa nafasi sahihi zinazopendekezwa kitaalamu, jambo linaloongeza idadi ya mimea inayostawi na kuongeza mavuno.
Kwa mfano, katika zao la alizeti, mkulima anayezingatia nafasi sahihi za upandaji anaweza kuvuna magunia 12 hadi 15 kwa ekari, ikilinganishwa na magunia matano hadi sita yanayoweza kupatikana kwa upandaji usiofuata viwango vinavyopendekezwa.
Faida nyingine ni kuwa mashine hiyo inaweza kuendeshwa na mwanaume au mwanamke, jambo linalowapa wanawake na vijana nafasi kubwa ya kushiriki katika kilimo cha kisasa na chenye tija.
Hii inaendana na azma ya Serikali ya kuongeza ushiriki wa vijana katika sekta ya kilimo kupitia matumizi ya teknolojia.
Kwa Malela, mafanikio ya Rafiki Planter ni ushahidi kuwa uwekezaji wa Serikali katika sayansi, teknolojia na ubunifu una matokeo yanayoonekana.
Anaamini kuwa kupitia COSTECH, wabunifu wengi wa Kitanzania wamepata fursa ya kubadili mawazo yao kuwa bidhaa na teknolojia zinazotoa suluhisho kwa changamoto za wananchi.
Kadiri COSTECH inavyoadhimisha miaka 40 tangu kuanzishwa kwake, simulizi ya Rafiki Planter inaonyesha kuwa maendeleo ya Taifa hayawezi kutenganishwa na uwekezaji katika sayansi, teknolojia na ubunifu.
Akizungumzia mchango wa Tume hiyo, Ofisa Mwandamizi wa COSTECH katika Mfuko wa Taifa wa Uendelezaji wa Sayansi na Teknolojia (MTUSATE), Ntufye Mwakigonja, anasema uwezeshaji wa ubunifu wa Rafiki Planter ni sehemu ya jukumu pana la COSTECH la kukuza teknolojia na ubunifu nchini.
Anasema tangu kufunguliwa kwa dirisha la ubunifu kupitia MTUSATE, COSTECH imetambua wabunifu zaidi ya 3,000 kutoka maeneo mbalimbali nchini, huku takribani wabunifu 350 wakiwezeshwa kupitia mafunzo, ufadhili wa kifedha na kuunganishwa na taasisi mbalimbali zinazochangia maendeleo ya teknolojia.
Akirejea safari ya Rafiki Planter, Mwakigonja anasema COSTECH ilitoa fedha zilizowezesha kuboresha teknolojia hiyo kutoka katika hatua ya awali ya sampuli kifani (prototype) iliyokuwa na uwezo mdogo hadi kufikia mashine yenye ufanisi mkubwa inayotumika na wakulima kwa sasa.

Kabla ya toleo la kwanza kulikuwa na teknolojua ya kukokotwa na wanyama kazi kama ng’ombe na punda
Hivyo safari ya Rafiki Planter si hadithi ya mashine pekee, bali ni ushahidi wa namna uwekezaji katika sayansi, teknolojia na ubunifu unavyoweza kubadili wazo rahisi kuwa suluhisho linaloboresha maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya Taifa.

