Na Lucy Ngowi
WAZIRI wa Maji, Jumaa Aweso, amewasilisha bajeti ya takriban Sh. Trilioni 1.2 kwa mwaka wa fedha 2026/2027, akieleza vipaumbele vitakavyoimarisha upatikanaji wa majisafi na salama kwa Watanzania.
Akiwasilisha hotuba hiyo Bungeni jijini Dodoma, amesema Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi na uendelezaji wa rasilimali za maji ili kuhakikisha usalama na upatikanaji wake kwa matumizi ya kijamii, kiuchumi na kimazingira.
Katika mwaka huo wa fedha, Wizara itakamilisha maandalizi ya Mpango Kabambe wa Taifa wa Maji pamoja na kuendeleza utekelezaji wa miradi ya Gridi ya Taifa ya Maji, inayolenga kusambaza maji kutoka vyanzo vya uhakika kama mito na maziwa kwenda maeneo yenye uhaba mkubwa.

Pia, Wizara itaongeza juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuimarisha uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua.
Mpango uliopo unahusisha ujenzi na ukarabati wa mabwawa 33, ubunifu wa mabwawa mapya 34, pamoja na tathmini ya athari za kimazingira kwa mabwawa mawili.
Wananchi pia watahamasishwa kuvuna maji ya mvua kupitia mapaa ya nyumba zao.
Katika kuboresha huduma, Wizara imepanga kukamilisha miradi 992 ya majisafi vijijini, miradi 196 mijini na miradi 26 ya usafi wa mazingira. Aidha, utekelezaji wa miradi mipya utaanza katika vijiji 314 kati ya 1,575 ambavyo bado havijafikiwa na huduma ya maji.
Waziri Aweso pia amesisitiza kudhibiti upotevu wa maji kwa kutumia teknolojia za kisasa kama mita za kielektroniki, mifumo ya usimamizi wa mtandao wa maji, na mita za malipo ya kabla. Hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya waharibifu wa miundombinu na wanaojihusisha na wizi wa maji.
Kipaumbele kingine ni kuhakikisha shule na vituo vya afya vinapata huduma ya maji na usafi wa mazingira.
Wizara itashirikiana na taasisi mbalimbali ikiwemo TAMISEMI kufanikisha azma hiyo.
Ili kufanikisha mipango hiyo, Wizara itatumia vyanzo mbadala vya fedha kama hati fungani, ushiriki wa sekta binafsi na fedha za mabadiliko ya tabianchi.
Pia itaendelea kuimarisha TEHAMA, rasilimali watu, pamoja na mifumo ya ufuatiliaji na tathmini ya miradi.
Bajeti hii inalenga kuharakisha upatikanaji wa majisafi na salama kwa wananchi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kukuza ustawi wa jamii na uchumi wa taifa.

