Naibu Katibu Mkuu (Taaluma) Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Dkt. Mwanakhamis Ameir (kulia) na Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Dkt. Erasmus Kipesha (kushoto) wakisaini mkataba maalum kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya elimu visiwani Unguja na Pemba.
Na Mwandishi Wetu
ZANZIBAR: MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA) na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar zimesaini mkataba maalum wa kushirikiana katika utekelezaji wa miradi ya elimu itakayohusisha ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya kujifunzia na kufundishia katika shule 20 za sekondari visiwani Unguja na Pemba.
Hafla ya utiaji saini imefanyika katika ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mazizini, Unguja ikiongozwa na Naibu Katibu Mkuu (Taaluma) Dkt. Mwanakhamis Ameir na Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Elimu Tanzania Dkt. Erasmus Kipesha.
Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Dkt. Erasmus Kipesha akisaini mkataba maalum wa kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya elimu visiwani Unguja na Pemba.
Akizungumza mara baada ya kusainiwa kwa mkataba huo Mkurugenzi Mkuu wa TEA, Dkt. Erasmus Kipesha amesema, jukumu kuu la mamlaka hiyo ni kutafuta rasilimali fedha na vifaa kutoka kwa wadau wa maendeleo ya sekta ya elimu ili kuboresha miundombinu ya elimu nchini.
Amebainisha kuwa tayari fedha zimepatikana kupitia wadau hao akiwemo UNICEF na kusisitiza umuhimu wa usimamizi madhubuti wa miradi hiyo ili ikamilike kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.
“Fedha tayari zipo kutoka kwa wadau wetu, hivyo ni wajibu wenu kuhakikisha miradi hii inatekelezwa ipasavyo na kukamilika kwa wakati,” amesema Dkt. Kipesha.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu (Taaluma) wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Dkt. Mwanakhamis Ameir, ameishukuru TEA kwa kuendelea kuwekeza katika kuboresha miundombinu ya elimu visiwani humo.
Amesema licha ya juhudi zinazofanywa na Serikali, bado kuna changamoto kubwa katika sekta hiyo hivyo ushirikiano huo ni muhimu katika kuzitatua.
Dkt. Ameir amesisitiza kuwa, wizara iko tayari kuanza utekelezaji wa miradi hiyo mara moja huku akiwataka wataalamu wote wanaohusika kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha miradi haikwamishwi.
“Ni muhimu kuthamini ushirikiano huu na kuhakikisha thamani ya fedha inayowekezwa inaonekana kupitia utekelezaji bora wa miradi,” ameongeza.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa awali na Mkurugenzi wa Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi ya Elimu Masozi Nyirenda, TEA inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya uboreshaji wa miundombinu ya elimu katika visiwa vya Unguja na Pemba.
Awali, takribani Sh. Bilioni 3.2 zilitengwa kwa ajili ya ujenzi wa shule za amali, huku Bilioni 2.5 zikielekezwa katika ujenzi na ukarabati wa vyumba vya madarasa, matundu ya vyoo na maabara za sayansi katika shule 20.