Kampuni ya Taifa Gas Tanzania imeendelea kuimarisha juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama nchini kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya gesi kwa taasisi, viwanda, hoteli na sekta ya utalii.

Akizungumza katika Maonyesho ya Kimataifa ya Karibu-KiliFair 2026, Meneja wa Mauzo wa Kitengo cha Wateja Wakubwa wa Taifa Gas, Moses Massawe, alisema kampuni hiyo imejipanga kuhakikisha nishati safi inawafikia Watanzania wote kuanzia ngazi ya kaya hadi taasisi kubwa.
Alieleza kuwa kitengo cha wateja wakubwa kinahudumia viwanda, shule, hoteli, migahawa, makampuni na taasisi mbalimbali zinazotumia gesi kama chanzo kikuu cha nishati.
“Kama Taifa Gas, tunaunga mkono juhudi za Serikali chini ya kampeni ya nishati safi inayohamasishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tunaamini taasisi zina nafasi kubwa katika kuongeza matumizi ya nishati safi nchini,” alisema.
Uwekezaji wa Miundombinu ya Gesi
Kwa mujibu wa Massawe, Taifa Gas imewekeza katika mifumo mbalimbali ya usambazaji wa gesi ikiwemo matenki yenye uwezo tofauti kulingana na mahitaji ya mteja.
Miundombinu hiyo imewezesha taasisi nyingi kubadilisha matumizi ya nishati za jadi na kuhamia kwenye gesi ambayo ni salama, nafuu na rafiki kwa mazingira.

Sekta ya Utalii Yapewa Kipaumbele
Taifa Gas imeeleza kuwa imefanikiwa kufikisha huduma zake katika maeneo mengi ya utalii nchini ikiwemo hifadhi za Serengeti, Tarangire, Ngorongoro na Manyara.
Kupitia huduma hizo, lodges, camps na hoteli zilizopo katika maeneo hayo sasa zinatumia nishati safi ya gesi kwa shughuli mbalimbali za kila siku.
Hatua hiyo inalenga kuunga mkono jitihada za uhifadhi wa mazingira pamoja na kuboresha huduma za utalii kwa kutumia nishati endelevu.
Teknolojia Mpya ya Digital Prepaid Meter
Katika maonyesho ya mwaka huu, Taifa Gas imezindua mfumo mpya wa Digital Prepaid Meter ambao unamwezesha mtumiaji kulipia kiwango halisi cha gesi anachotumia.
Mfumo huo unatarajiwa kuleta mapinduzi makubwa katika usimamizi wa matumizi ya gesi kwa wamiliki wa apartment, kambi za taasisi, makazi ya pamoja na majengo yenye watumiaji wengi.
Kwa kutumia teknolojia hiyo, kila mtumiaji ataweza kufuatilia matumizi yake na kulipia kiwango alichotumia pekee bila kubebeshwa gharama za watumiaji wengine.

Huduma Zafika Mikoa Yote Tanzania
Taifa Gas imesema imefanikiwa kuanzisha maghala na vituo vya usambazaji katika mikoa mbalimbali nchini ili kuhakikisha upatikanaji wa gesi unakuwa wa haraka na wa uhakika kwa wateja wote.
Kampuni hiyo imewahakikishia wadau wa sekta ya utalii, viwanda na taasisi mbalimbali kuwa itaendelea kuboresha huduma zake na kuwekeza katika teknolojia mpya zinazorahisisha matumizi ya nishati safi nchini Tanzania.
Kwa mujibu wa kampuni hiyo, lengo kuu ni kuona Watanzania wengi zaidi wakihamia katika matumizi ya nishati safi na salama kwa maendeleo endelevu ya taifa na uhifadhi wa mazingira.

