Na Lucy Ngowi
DODOMA: MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) imeendelea kuimarisha utoaji wa huduma kwa kuzingatia uwajibikaji, uwazi na weledi, sambamba na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kuboresha usafiri wa anga na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa TAA, Irene Minja, wakati wa Maadhimisho na Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Minja amesema kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu isemayo “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu” inaakisi dhamira ya TAA ya kuhakikisha wananchi na wadau wanapata huduma bora, salama na zenye ufanisi mkubwa.

Amefafanua kuwa TAA ni taasisi ya Serikali yenye jukumu la kujenga, kuendeleza, kusimamia na kuendesha viwanja vya ndege vya Serikali Tanzania Bara, na kwamba imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya sekta ya usafiri wa anga.
Kwa mujibu wa Minja, maboresho ya miundombinu ya viwanja vya ndege yana mchango mkubwa katika kukuza biashara, utalii na uwekezaji, huku yakirahisisha usafirishaji wa watu na mizigo ndani na nje ya nchi.
Amesema viwanja vya ndege vinaendelea kuwa lango muhimu la kuunganisha Tanzania na mataifa mbalimbali duniani, hivyo uwekezaji unaofanywa katika sekta hiyo unalenga kuimarisha ushindani wa nchi na kuvutia fursa zaidi za kiuchumi.
“Tunatambua mchango mkubwa wa viwanja vya ndege katika maendeleo ya taifa. Ndiyo maana tunaendelea kuboresha huduma na miundombinu ili kuhakikisha Tanzania inakuwa kivutio kikubwa cha watalii, wafanyabiashara na wawekezaji kutoka maeneo mbalimbali duniani,” amesema.
Aidha, amewahimiza wananchi kutembelea banda la TAA katika maonesho hayo ili kupata taarifa sahihi kuhusu huduma zinazotolewa na mamlaka hiyo, kujifunza kuhusu miradi ya maendeleo inayotekelezwa na kutoa maoni yatakayosaidia kuboresha zaidi utoaji wa huduma kwa umma.
Amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya wananchi na taasisi za umma ni muhimu katika kufanikisha utoaji wa huduma bora na maendeleo endelevu ya taifa.

