Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MKUU wa Wilaya ya Kondoa, Fatma Almas Nyangasa, ameipongeza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa matumizi ya teknolojia za kisasa katika usimamizi wa misitu na uendelezaji wa utalii, akisema hatua hiyo inaongeza ufanisi wa uhifadhi na kuvutia watalii kutembelea vivutio vya Tanzania.
Nyangasa ametoa pongezi hizo alipotembelea banda la Wizara ya Maliasili na Utalii katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea Viwanja vya Nzuguni, Dodoma, ambapo alipata maelezo kuhusu shughuli na huduma zinazotolewa na TFS kwa mujibu wa majukumu yake ya kisheria.

Akiwa katika banda la TFS, amejionea matumizi ya ndege zisizo na rubani (drones) katika usimamizi wa misitu pamoja na teknolojia ya Virtual Reality inayowawezesha wananchi na wageni kutembelea vivutio vya utalii kwa njia ya mtandao kabla ya kufika maeneo husika.
Amesema matumizi ya teknolojia hizo ni hatua muhimu ya kuimarisha uhifadhi wa rasilimali za misitu na kuongeza hamasa ya watalii kutembelea maeneo yenye vivutio mbalimbali, ikiwemo Eneo la Urithi wa Dunia la Michoro ya Miambani ya Kondoa.
Ameongeza kuwa, ubunifu unaoendelea kufanywa na TFS unapaswa kuendelezwa kwa kuwa unarahisisha utoaji wa elimu kwa wananchi na kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii wa asili na urithi wa kiutamaduni.


