Na Lucy Lyatuu, Dodoma
TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) inaendeea kuhamasisha wananchi kujua hali zao za afya kupitia kampeni ya “Jua Namba Zako”, inayofanyika katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwenye Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea banda la JKCI, Meneja wa Huduma na Utawala wa taasisi hiyo, Josephat Asenga, amesema kampeni hiyo inalenga kuwahamasisha wananchi kufahamu viashiria muhimu vya afya ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.
Kwa upande wake, Dkt Daud Bwilenza amesema hadi kufikia siku ya tatu ya maadhimisho hayo, JKCI imehudumia watu 170 waliopimwa magonjwa ya moyo, umeme wa moyo na kisukari, huku zaidi ya wagonjwa 20 wakipewa rufaa kwa uchunguzi na matibabu ya kina.

Dkt. Bwilenza amesema ongezeko la magonjwa ya moyo na kisukari linachangiwa na sababu zinazoweza kuzuilika ikiwemo kutofanya mazoezi, ulaji usiozingatia lishe bora na kutofanya uchunguzi wa afya mara kwa mara.
Ametoa wito kwa wakazi wa Dodoma na wananchi wote wanaotembelea maadhimisho hayo kufika katika banda la JKCI kupima afya zao, kupata ushauri wa kitaalamu na huduma za matibabu ili kubaini changamoto za kiafya mapema na kuanza matibabu kwa wakati.

