MWANZA: NAIBU Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Rose Ambrose, amesema kazi ya uhifadhi na uendelezaji wa Ziwa Victoria inahitaji fedha za kutosha, utangamano pamoja na ushirikiano wa karibu katika ngazi zote, kutokana na ukweli kwamba changamoto za maji duniani zimeongezeka na kuvuka mipaka ya kiutawala.
Rose Ambrose ameyasema hayo wakati akifungua warsha ya wadau wa Bonde la Ziwa Victoria, iliyofanyika jijini Mwanza ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya kwanza ya Ziwa Victoria.
Amesema changamoto hizo ni pamoja na upungufu wa maji, ukame, mafuriko, uchafuzi wa mazingira na athari za mabadiliko ya tabianchi, hali inayohitaji juhudi za pamoja kati ya mataifa na wadau mbalimbali.

Kutokana na hali hiyo, amewaalika wadau wa maendeleo kuwekeza katika uhifadhi na usimamizi endelevu wa rasilimali za maji za Ziwa Victoria ili kuhakikisha uhai wake unadumu kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.
Ameeleza kuwa usimamizi wa rasilimali za maji unahitaji mshikamano wa jamii na mataifa, akisisitiza kuwa maji ni kiungo muhimu cha kuunganisha watu.
“Maji yanalazimisha jamii kuungana na kushirikiana,” amesema.
Aidha, ametoa wito kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, jumuiya ya kimataifa, washirika wa maendeleo, wataalamu, watafiti, asasi za kiraia na wadau wengine kushiriki kikamilifu katika juhudi za kulinda na kuhifadhi Ziwa Victoria.

“Kila mmoja akiwa balozi mzuri wa uhifadhi wa Ziwa Victoria kwa kufanya shughuli za kulinda mazingira na kuzuia shughuli hatarishi, tutafanikiwa,” ameongeza.
Warsha hiyo imehudhuriwa na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi, ikiwa na kaulimbiu isemayo, “Maji Yetu, Mustakabali Wetu, Tuungane kwa Usimamizi Endelevu wa Bonde la Ziwa Victoria’.

