Na Lucy Lyatuu, Dodoma
WIZARA ya Ujenzi imeliomba Bunge kuiidhinishia Sh trilioni 2.5 kwa mwaka wa fedha 2026-2027 kwa ajili ya kutekeleza Vipaumbele sita ambavyo vitajikita katika ujenzi wa miundombinu na barabara.
Aidha imesema Serikali itaendelea na ujenzi pamoja na ukarabati wa barabara kuu na za mikoa kwa kiwango cha lami na changarawe ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kurahisisha huduma za usafirishaji kwa wananchi.
Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amesema hayo bungeni wakati akiwasilisha bajeti ya wizara hiyo na kuongeza kuwa Serikali itaendelea kuwekeza katika ujenzi wa madaraja makubwa na ya kimkakati pamoja na kuimarisha mtandao wa barabara ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za usafiri katika maeneo yote ya nchi.

Amesema miradi hiyo inalenga kupunguza changamoto za usafiri hususan katika maeneo yanayokumbwa na kukatika kwa mawasiliano wakati wa mvua, kupunguza gharama za usafirishaji na kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa bidhaa na huduma.
Ulega amesema Serikali pia itaendelea kujenga miundombinu yenye uwezo wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kutumia teknolojia na viwango vya kisasa katika ujenzi wa madaraja, barabara na vivuko.
Aidha, amesema uwekezaji katika miundombinu utafungua fursa zaidi za kiuchumi kwa kuunganisha maeneo ya uzalishaji na masoko, kuimarisha sekta za kilimo, utalii, biashara na viwanda pamoja na kuongeza ushindani wa Tanzania katika biashara za kikanda na kimataifa.

Amesema lengo ni kuwa na miundombinu ya kisasa, salama na yenye kuaminika ambayo itaendana na kasi ya ukuaji wa uchumi na mahitaji ya wananchi.
Kuhusu vipaumbele amesema serikali itaendelea na ujenzi wa madaraja makubwa, madaraja madogo na makalavati katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kuimarisha mawasiliano na usafiri kati ya mikoa na wilaya.
Aidha, wizara hiyo itaendelea kufanya matengenezo ya barabara na madaraja yaliyopo ili kuhakikisha miundombinu hiyo inakuwa salama, imara na kudumu kwa muda mrefu kwa watumiaji wote wa barabara.
Ulega amesema kipaumbele kingine ni kukamilisha miradi ya dharura ya miundombinu iliyoharibiwa na mvua za El-Nino pamoja na Kimbunga Hidaya ili kurejesha huduma za usafiri katika maeneo yaliyoathirika.

Waziri huyo amesema pia wizara itaendelea kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa miradi mipya ya barabara na madaraja ili kuweka msingi wa utekelezaji wa miradi mikubwa ya baadaye.
Pamoja na hilo, Serikali imeweka mkazo katika kupunguza msongamano wa magari katika majiji makubwa hususan Dar es Salaam na Dodoma kupitia upanuzi wa barabara, ujenzi wa flyovers na barabara za mzunguko.

