Na Lucy Lyatuu
CHAMA cha Wakunga Tanzania (TAMA) kimetangaza kuadhimisha Siku ya Mkunga Duniani kuanzia Mei 2 hadi 5 mwaka huu mkoani Kilimanjaro, huku kikionya juu ya upungufu mkubwa wa wakunga unaoendelea kuhatarisha maisha ya akina mama na watoto wachanga.
Akizungumza na Waandishi wa habari Dar es Salaam Leo Rais wa TAMA, Beatrice Mwilike amesema takwimu zinaonesha kuwa bara la Afrika linakabiliwa na upungufu wa takribani wakunga 460,000, hali inayochangia ongezeko la vifo vya mama na mtoto, hasa katika maeneo yenye changamoto za majanga na huduma duni za afya.
Amesema mbali na uhaba huo, vituo vingi vya kutolea huduma za afya vinakumbwa na changamoto za miundombinu na mazingira yasiyo rafiki kwa wakunga, ikiwemo ukosefu wa maji safi, vyoo bora na mazingira salama ya usafi binafsi, hali inayohatarisha usalama wa mama na mtoto wakati wa kujifungua.
“Upungufu wa wakunga si takwimu tu, bali ni maisha ya akina mama na watoto yaliyo hatarini kila siku. Tunahitaji uwekezaji wa haraka, mafunzo zaidi na kuboresha mazingira ya kazi ili kuhakikisha uzazi salama,” amesema Mwilike.
Ameeleza kuwa maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kauli mbiu isemayo “Dunia inahitaji wakunga milioni moja zaidi”, yakilenga kuongeza idadi ya wakunga pamoja na kuimarisha huduma za afya ya uzazi.

Kwa mujibu wa Mwilike, shughuli zitakazofanyika ni pamoja na mbio za “Mkunga Half Marathon”, maonesho ya huduma za afya kwa jamii, pamoja na mafunzo maalum kwa wakunga ili kuongeza ujuzi na weledi katika taaluma hiyo.
Ameongeza kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa wakunga, kuchochea uwekezaji na sera bora, pamoja na kukusanya rasilimali zitakazosaidia kuboresha huduma za afya ya uzazi nchini.
Kwa upande wake, Muuguzi Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Joyce Muna amesema bado kuna upungufu mkubwa wa watoa huduma za afya, jambo linaloathiri utoaji wa huduma bora kwa mama na mtoto.
“Tunatoa wito kwa wauguzi na wakunga kujitokeza kushiriki mbio hizi, kwani ni fursa ya kuchangia upatikanaji wa vifaa tiba vitakavyosaidia kuokoa maisha ya mama na mtoto. Wakunga ni nguzo muhimu ya uzazi salama na ndio wanaompokea mtoto mara ya kwanza anapozaliwa,” amesema Muna.
Naye Mratibu wa Chama cha Wakunga kutoka Canada, Stephano Simba ameipongeza TAMA kwa maandalizi ya maadhimisho hayo, akibainisha kuwa wanaendelea kushirikiana katika miradi ya uzazi salama kwa lengo la kuwajengea uwezo wakunga wanafunzi na wataalamu wa afya.
Amesema ushirikiano huo unalenga kuongeza ujuzi na stadi kwa watoa huduma za afya ili kuboresha huduma na kupunguza vifo vya mama na mtoto, huku akisisitiza umuhimu wa wadau na serikali kuendelea kuwekeza katika sekta hiyo muhimu.

