Anaeleza kuwa teknolojia hiyo hutumia ndizi kali ambazo huchanganywa na majani maalum, kisha kusagwa kwa kutumia mikono au miguu katika hatua za awali za uzalishaji wa juisi. Juisi, baada ya kuchachuka kwa takribani siku mbili hupatikana pombe ya asili ijulikanayo nama Rubisi.
“Hapo awali, njia ya kutengeneza ilikuwa na changamoto za usafi kwa sababu ilihusisha kukanyaga kwa miguu, lakini hilo ndilo lililonisukuma kuendeleza utafiti zaidi baada ya masomo yangu ya shahada ya pili na ya tatu ili kuboresha teknolojia hii,” anasema Profesa Kibazoli.
Anafafanua kuwa kile kinachojulikana kama togwa ya ndizi ni tofauti na juisi ya ndizi anayoifanyia utafiti, akibainisha kuwa juisi hiyo ni kinywaji chepesi chenye maji mengi na si uji mzito.
Kwa mujibu wa utafiti wake, juisi hiyo hutokana na ndizi kali zenye utomvu mkali, ambazo zikichemshwa hupata rangi ya kahawia na ladha tofauti na matoke ya kawaida.
Teknolojia mpya ilivovumbuliwa na Profesa Kibazohi inatumai machine za kisasa. Anaongeza kuwa kwa sasa wamepiga hatua na wanaweza kuzalisha juisi hiyo kwa kutumia mashine za kisasa badala ya mbinu za jadi za kuchanganya na majani na “kukanda” kwa mikono au kukanyaga kanyaga kwa miguu.
Anaongeza kuwa utekelezaji wa teknolojia hiyo unahitaji wataalamu mbalimbali kama vile wataalamu wa uzalishaji kiviwanda, wataalamu wa masoko na uuzaji, pamoja na uwekezaji mkubwa wa kifedha ili kuifanya iweze kufikia soko la kitaifa na kimataifa.
Kwa upande wa uchumi, Profesa Kibazoli anasema teknolojia hiyo inaweza kuongeza thamani ya mgomba wa ndizi, kuongeza kipato cha wakulima na kufungua nafasi za ajira katika mnyororo mzima wa uzalishaji, usindikaji na usambazaji.
Anaeleza kuwa juisi hiyo ina kiwango kikubwa cha sukari, ambapo hupunguzwa kwa kuchanganywa na maji safi hadi kufikia kiwango kinachokubalika cha takribani asilimia 13.
Akihusisha na Dira ya Taifa 2050, Profesa huyo anasema maendeleo ya viwanda vya ndani vya vinywaji ni sehemu muhimu ya kujenga uchumi imara unaojitegemea, badala ya kuendelea kuagiza juisi kutoka nje ya nchi.
“Tanzania inaweza kuzalisha juisi yake, ikatumia bidhaa zake na hata kuuza nje ya nchi. Hii itasaidia kuajiri Watanzania wengi na kuongeza mzunguko wa fedha ndani ya nchi,” anasema.
Aidha, anasisitiza umuhimu wa kuongeza mafunzo ya vitendo katika elimu ya uhandisi na sayansi, akibainisha kuwa utafiti wa ndani unapaswa kulenga kuendeleza rasilimali zilizopo nchini badala ya kutegemea mifumo ya nje pekee.
Anaeleza kuwa hata katika sekta kama uhandisi wa mafuta na gesi, kuna fursa ya kutumia maarifa hayo katika uzalishaji wa bidhaa nyingine kama mbolea na bidhaa za viwandani zinazoweza kuingizwa kwenye mitaala ya elimu na kuleta ajira zaidi.
Kwa mujibu wake,
maendeleo ya teknolojia hiyo yanaweza kuchochea uzalishaji wa viwandani, kuongeza ajira za madereva, wataalamu wa masoko, mafundi na wakulima, hivyo kuchangia moja kwa moja katika maendeleo ya taifa kuelekea uchumi wa viwanda unaokusudiwa katika Dira ya 2050.
Tafiti mbalimbali za kilimo na teknolojia ya chakula katika Ukanda wa Afrika Mashariki zinaonyesha kuwa ndizi aina ya plantain na ndizi kali zina uwezo mkubwa wa kuchakatwa kuwa bidhaa mbalimbali ikiwemo juisi, unga na vinywaji vya uchachushaji.
Ripoti za Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) zinaeleza kuwa kuongeza thamani ya mazao ya ndizi ni njia muhimu ya kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvunwa na kuongeza kipato cha wakulima wadogo.
Aidha, tafiti za teknolojia ya uchachushaji zinaonesha kuwa mchakato wa kubadili ndizi kuwa kinywaji ni wa muda mrefu katika baadhi ya jamii za Afrika Mashariki, ambapo matumizi ya vifaa vya kisasa yanaweza kuboresha usafi, ubora na uzalishaji wa kiwango cha viwandani.
Katika nyanja ya uchumi wa viwanda, ripoti za maendeleo zinaeleza kuwa sekta ya usindikaji wa mazao ya kilimo ni mhimili muhimu wa kufanikisha ajenda za viwanda na ajira, hususan katika nchi zinazoendelea.
Hii inaendana na malengo ya Dira ya Taifa 2050 yanayolenga kuongeza uzalishaji wa ndani, kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje na kukuza ajira kupitia viwanda vya ndani.
Pia imebainika kuwa uwekezaji katika teknolojia za usindikaji wa chakula na vinywaji huongeza mnyororo wa thamani unaowahusisha wakulima, wasindikaji, wasafirishaji na wauzaji, hivyo kuchochea mzunguko mpana wa kiuchumi na kuongeza ajira katika sekta mbalimbali.