Zaidi ya Bilioni 1.6 Zaahidiwa
Na Lucy Ngowi
DODOMA: Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwinjulu Nchemba, ameongoza hafla ya uchangishaji fedha kwa ajili ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) mwaka 2026, yatakayofanyika kitaifa mkoani Njombe, huku wadau mbalimbali wakiahidi kuchangia zaidi ya Shilingi bilioni 1.6.
Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Nchemba amesema Maadhimisho ya Mei Mosi ni jukwaa muhimu la kutambua mchango wa wafanyakazi katika maendeleo endelevu ya taifa, akibainisha kuwa mafanikio ya sekta mbalimbali yanatokana na juhudi zao.
“Tunatambua kazi kubwa inayofanywa na wafanyakazi wa sekta za umma na binafsi. Mei Mosi si tukio la kawaida la kalenda, bali ni siku ya kuenzi mafanikio yanayotokana na juhudi zao kupitia Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA),” amesema.

Ameongeza kuwa mafanikio hayo yanachangiwa na uwajibikaji wa wafanyakazi katika sekta zote, huku akisisitiza umuhimu wa wadau kuendelea kuunga mkono maandalizi ya sherehe hizo.
Dkt. Nchemba amempongeza Waziri wa Kazi, Ajira na Mahusiano ya Viwanda, Deus Sangu, kwa kusimamia vizuri maandalizi hayo na kuweka msukumo katika kufanikisha shughuli hiyo.
Amesema fedha zitakazopatikana zitatumika kugharamia maandalizi ya maadhimisho hayo, na kuwataka wadau kuendelea kujitokeza kwa wingi kuunga mkono jitihada hizo.
Miongoni mwa taasisi zilizotoa ahadi za michango ni Benki ya CRDB (Sh. milioni 100), Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Sh. milioni 10, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Sh. milioni 10, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) Sh. milioni 30, Benki ya NMB Sh. milioni 80 na Benki ya Azania Sh. milioni 20.

Wengine ni Bodi ya Mkonge Tanzania (Sh. milioni 20), Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) Sh. milioni 10, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Sh. milioni 20, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) Sh. milioni 35, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Sh. milioni 30 na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Sh. milioni 50.
Pia, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) Sh. milioni 20, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Sh. milioni 100, Benki ya Ushirika Tanzania (TCB) Sh. milioni 10, Shirika la Viwango Tanzania (TBS) Sh. milioni 10 na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Sh. milioni 100 walijumuika katika michango hiyo.

Taasisi nyingine ni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Sh. milioni 100, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Ushirika Sh. milioni 20, Wakala wa Serikali Mtandao (e-GA) Sh. milioni 30, taasisi zilizo chini ya Wizara ya Kazi, Ajira na Mahusiano Sh. milioni 150 pamoja na Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Sh. milioni 150.

Kwa upande wake, Waziri wa Kazi, Ajira na Mahusiano Sangu, amesema uwepo wa Waziri Mkuu katika hafla hiyo ni ishara ya dhamira ya Serikali katika kuimarisha ustawi wa wafanyakazi na taifa kwa ujumla.
Amesema maandalizi ya Maadhimisho ya Mei Mosi yanaendelea vizuri, ikiwemo uboreshaji wa miundombinu ya uwanja utakaotumika, huku wakitarajia kushirikisha zaidi ya watu 5,000.
Amebainisha kuwa bajeti ya maandalizi hayo ni takribani Sh. Bilioni 5.

Naye Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Tumaini Nyamhokya, amesema vyama vya wafanyakazi vitaendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha maadhimisho hayo yanafanyika kwa mafanikio makubwa, akisisitiza ushirikiano huo utaongeza tija kwa wafanyakazi na taifa kwa ujumla.


