Tanzania Yataka Walimu Wasibaki Watumiaji Wa Teknolojia, Wazalishe Pia
Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: TAKRIBANI walimu 600 kutoka shule za msingi na sekondari pamoja na wahadhiri wa vyuo vikuu nchini wameshiriki mashindano ya Umahiri kwa Walimu wa Tanzania katika matumizi ya teknolojia za kidijitali, huku Serikali ikisisitiza umuhimu wa walimu kutumia teknolojia na Akili Bandia (AI) kuboresha ufundishaji na ujifunzaji.
Mashindano hayo, yaliyoanza katikati ya Juni na kukamilika katikati ya Agosti 2026, yamelenga kuwajengea walimu uwezo wa kutumia zana za kidijitali, AI, kuandaa mipango ya masomo, kuunda rasilimali za kufundishia na kubuni mbinu bora za ufundishaji.
Akizungumza katika hafla ya kuwatunuku washindi wa mashindano hayo, Mkuu wa Shule ya Elimu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dkt. Nkanileka Mgonda, amesema mashindano hayo yameandaliwa kwa ushirikiano kati ya UDSM na Chuo Kikuu cha Zhejiang Normal cha China (ZJNU), kwa kushirikisha Tanzania AI Community.
Amesema washiriki walipitia hatua tatu, ambapo awali walijisajili kupitia mfumo maalumu na kuandaa mipango ya masomo iliyojumuisha matumizi ya teknolojia za kidijitali, hususan AI.
“Baadaye, walimu waliwasilisha video za ufundishaji, ambapo zaidi ya 200 walifanikiwa kuwasilisha kazi zao. Kazi hizo zilitathminiwa na majaji 15, wakiwemo 10 kutoka Tanzania na watano kutoka China,” amesema.
Kwa mujibu wa Dkt Mgonda, baada ya tathmini, walimu 90 walichaguliwa kwa hatua ya mwisho iliyofanyika UDSM, ambako walifundisha masomo halisi mbele ya majaji.
Amesema tathmini ilizingatia matumizi ya teknolojia, ubunifu, matumizi ya AI na ufanisi wa mbinu za ufundishaji, kabla ya kuchaguliwa washindi watano bora.
Aidha, walimu 90 waliofika hatua ya mwisho watapatiwa mafunzo ya siku tatu kuhusu matumizi ya teknolojia za kidijitali na AI katika elimu, hatua inayolenga kuendeleza ujuzi walioupata kupitia mashindano hayo.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa wizara hiyo, Profesa Ladislaus Mnyone, amesema Tanzania inaendelea kuwekeza katika teknolojia mbalimbali, ikiwemo teknolojia zinazoibukia kama AI, ili kuboresha ufundishaji, ujifunzaji na usimamizi wa elimu.
Amesema mpango huo unaendana na mipango ya kimkakati ya nchi pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayosisitiza matumizi ya teknolojia za kidijitali.
“Moja ya nyenzo za Dira ya Taifa ni matumizi ya kidijitali. Ikiwa walimu wetu wameandaliwa vizuri katika shule za msingi, sekondari na vyuo, wanafunzi watakaowaandaa watakuwa na uelewa, ujuzi na fursa ya kutumia teknolojia hiyo katika sekta mbalimbali,” amesema.
Profesa Mnyone amesema Tanzania haitaki kubaki kuwa mtumiaji wa teknolojia pekee, bali inalenga kujenga uwezo wa kuzalisha teknolojia zake.
“Tunategemea kama nchi tusiwe tu watumiaji wa teknolojia ya kidijitali, bali pia wazalishaji wa teknolojia hizo,” amesema.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Zhejiang Normal, Profesa Xiao Huang, amesema mashindano hayo siyo tu sherehe ya kutambua mafanikio ya walimu, bali ni mwanzo wa safari mpya ya kuimarisha elimu barani Afrika na kukuza ushirikiano kati ya Afrika na China katika sekta hiyo.
Amewapongeza walimu waliotunukiwa tuzo pamoja na washiriki wote, akisema wameonesha ubunifu na ujasiri wa kutumia mbinu mpya katika ufundishaji.
“Nawapongeza kwa maandalizi yenu, ubunifu wenu na ujasiri wa kutumia mbinu mpya katika ufundishaji,” amesema.
Ametoa pia shukrani kwa mamlaka za elimu, UDSM, walimu na wadau wengine waliochangia kufanikisha mashindano hayo.
Mmoja wa washindi wa mashindano hayo, Mwinyiheri Zuberi, ambaye ni mwalimu kutoka mkoani Kigoma, amesema ushindi huo utamchochea kutumia zaidi teknolojia katika kuboresha ufundishaji wake.
Hata hivyo, amesema changamoto kubwa katika baadhi ya shule ni upatikanaji wa vifaa vya teknolojia.
Amesema katika Shule ya Buyungi anayofundisha, kwa sasa anatumia kompyuta moja inayounganishwa na spika ili kuwafikia wanafunzi wengi kwa wakati mmoja.
“Malengo ni kuona kunakuwa na kompyuta nyingi ili watoto wengi waweze kuona kwa macho kile wanachofundishwa,” amesema.



