Na Lucy Lyatuu, Morogoro
BODI Ya Rufani za Kodi (TRAB) imesema imetumia Tamasha la Nne la Kitaifa la Utamaduni linalofanyika mkoani Morogoro kuelimisha wananchi hatua wanazoweza kuchukua iwapo hawajaridhishwa na masuala ya kikodi.
Aidha imetoa elimu kuhusu taratibu, haki na wajibu wa mlipa kodi, hususan namna ya kukata rufaa dhidi ya maamuzi ya kikodi.
Ofisa kutoka TRAB, Mabel Nasua, amesema elimu hiyo inalenga kuwawezesha wananchi kuelewa ni taratibu gani zinazotakiwa kufuatwa iwapo atakuwa na changamoto yoyote ya kikodi.


Ameeleza kuwa TRAB pia imekuwa ikitoa ufafanuzi kuhusu gharama zinazohusiana na mchakato wa rufaa, ambapo wananchi wanapaswa kufahamu ada mbalimbali zinazotozwa katika hatua za kuwasilisha na kusikiliza rufaa zao.
Aidha, amesisitiza kuwa mtu anayekata rufaa anatakiwa kufuata taratibu zilizowekwa na Sheria ya Rufani za Kodi, ikiwemo kuwasilisha nyaraka zinazohitajika na kuhudhuria mchakato wa usikilizwaji wa shauri lake.
Kwa mujibu wa Nasua Kutofuata masharti hayo kunaweza kuathiri rufaa yake.
Kadhalika amesema mlipa kodi anayepinga uamuzi wa mwisho wa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) anaweza kukata rufaa kwa kuwasilisha kusudio la kukata rufaa kwa maandishi ndani ya siku 30 tangu siku aliyopokea notisi ya uamuzi huo.


Hata hivyo TRAB imewahimiza wananchi kutumia fursa ya elimu inayotolewa katika matamasha na maonesho mbalimbali ili kufahamu haki zao za kikodi na namna sahihi ya kuzitetea, huku ikisisitiza umuhimu wa wananchi kupata ushauri na kufuata taratibu rasmi badala ya kukata tamaa wanapokumbana na changamoto za kikodi.



