Na Lucy Lyatuu, Dodoma
WAKALA wa Barabara Vijijini Na Mijini (TARURA) umesema kuelekea utekelezaji wa dira 2050 inawapatia ajira vikundi vya vijana, wanawake na walemavu ambapo inatoa elimu kwa wananchi waweze kufanya kazi za barabara .
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano Na Mawasiliano TARURA, Catherine Sungura amesema hayo wakati akizungumza katika banda la Wakala huo, lililopo katika wiki ya utumishi wa umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park mkoani Dodoma.
Amesema programu hiyo ni ya nchi nzima kasoro mkoa wa Dar es Salaam na imeanza katika miaka miwili iliyopita ambapo kupitia elimu wamewafikiwa vikundi vya vijana,wanawake na walemavu.
Amesema kupitia vikundi hivyo, husajiliwa kwenye mfumo wa NeST na iwapo ikitokea zabuni ya ujenzi wa barabara au madaraja hupewa kazi za matengenezo madogomadogo kwa mwaka mara moja.

“Kama wamepewa barabara fulani huifanyia matengenezo madogomadogo,hata kama kuna mfereji wenye mchanga hupewa zabuni waifanye kwa mwaka mzima,” amesema Catherine huku akitolea mfano kikundi cha waendesha bodaboda kilichoko Ifakara kuwa kimeweza kujinufaisha kwa program hiyo.
Amesema kikundi hicho kimepata takriban sh milioni 13 kwa kusafisha barabara ambayo ni fursa ya ajira kwa vijana, hivyo anatoa wito kwa wananchi kujiunga na kuchangamkia fursa hiyo
Catherine amesema mfano mwingine ni kikundi kilichopo Ludewa ambapo kilianza siku nyingi kwa kujenga barabara wameweza kununua pikipiki, kuweka mizinga ya asali ambapo hukopeshana na kuongeza mitaji.
Kwa upande wake Ofisa Utumishi Mkuu wa TARURA, Speransia Mhapa amesema wakala huo umefanikiwa kufungua nchi katika maeneo mbalimbali kwa ujenzi wa barabra na kutoa huduma.
Amewakaribisha wananchi katika banda hilo waulize na kutoa mirejesho ya kazi za wakala huo na kuiwezesha Tarura kujifanyia tathmini kuhusu huduma watoazo.

