Na Lucy Ngowi
DODOMA: Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, ameipongeza Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwa mchango wake katika kuimarisha sekta ya elimu nchini kupitia usimamizi wa Mfuko wa Elimu wa Taifa na utoaji wa elimu kwa umma kuhusu shughuli zake.
Pongezi hizo alizitoa jana alipotembelea banda la TEA katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Akiwa katika banda hilo, Kikwete amesema anatambua kazi kubwa inayofanywa na TEA katika kuisaidia Serikali kuboresha elimu kwa kutafuta vyanzo vya rasilimali fedha na vifaa vinavyosaidia kuimarisha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.
“Nazifahamu kazi zinazofanywa na TEA. Endeleeni kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yenu ili watu wengi zaidi waweze kufahamu mchango wa mamlaka hii katika maendeleo ya elimu nchini,” amesema Kikwete.
Awali, Ofisa Uhusiano wa TEA, Eliafile Solla, amesema mamlaka hiyo inasimamia Mfuko wa Elimu wa Taifa wenye jukumu la kutafuta na kuhamasisha upatikanaji wa rasilimali fedha na vifaa kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya elimu nchini.
Amefafanua kuwa rasilimali hizo husambazwa katika shule na taasisi mbalimbali za elimu kwa lengo la kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, hivyo kuongeza ubora na upatikanaji wa elimu kwa usawa.
“TEA ni taasisi ya Serikali iliyo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Tumeshiriki maonesho haya ili kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yetu na miradi mbalimbali inayotekelezwa kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa,” amesema Solla.
Ameongeza kuwa watumishi wa TEA wamejipanga kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hususan katika kutafuta rasilimali zitakazosaidia juhudi za Serikali za kuboresha sekta ya elimu nchini.

