Na Lucy Ngowi
DODOMA: WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, ametembelea banda la Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na kujionea utekelezaji wa miradi ya usambazaji wa umeme pamoja na matumizi ya mifumo ya kidigitali inayorahisisha upatikanaji wa taarifa kwa wananchi.
Akiwa katika banda hilo, Ridhiwani amepata maelezo kutoka kwa Ofisa Upimaji Mwandamizi wa REA, Hussein Shamba, aliyemueleza maendeleo ya usambazaji wa umeme katika vitongoji nchini na mafanikio ya matumizi ya mfumo wa kidigitali wa ufuatiliaji wa miradi hiyo.

Shamba amesema kasi ya usambazaji wa umeme vijijini imefikia asilimia 77, ambapo jumla ya vitongoji 39,840 tayari vimefikiwa na huduma ya umeme.
Amebainisha kuwa vitongoji 12,736 vilivyobaki vinatarajiwa kukamilishwa ifikapo mwaka 2030/2031.
“Kwa sasa tupo katika hatua ya juu ya utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini, na tunatarajia kukamilisha vitongoji vyote vilivyobaki ndani ya muda uliopangwa,” amesema Shamba.
Aidha, amefafanua kuhusu mfumo wa kidigitali unaowawezesha wananchi kupata taarifa mbalimbali za huduma ya umeme kupitia simu zao za mkononi, ikiwa ni pamoja na hali ya upatikanaji wa umeme katika maeneo yao.
Amemwonesha Waziri mfano wa Mkoa wa Pwani, Wilaya ya Bagamoyo, Jimbo la Chalinze, ambapo mfumo huo umeonyesha kuwa vijiji 286 vina umeme, vijiji 133 vipo kwenye mpango wa utekelezaji, huku vitongoji 50 vikiwa katika hatua ya utekelezaji wa wakandarasi waliopo maeneo ya kazi.
Mfumo huo pia unaonesha kwa uwazi vitongoji vyote vilivyofikiwa na umeme pamoja na vile vilivyo kwenye mpango wa kufikishiwa huduma hiyo, hatua inayolenga kuongeza uwazi na ufanisi katika utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini.
Katika hatua nyingine, Ridhiwani ameoneshwa matumizi ya nishati safi ya kupikia, ambapo alikabidhiwa jiko la sahani mbili kwa ajili ya kuendelea kutoa hamasa na kuwa mfano katika matumizi ya nishati hiyo katika jamii mbalimbali nchini.

