Na Lucy Lyatuu, Dodoma
TAASIS ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) imesema takwimu zinaonyesha katika kila watoto 10 kwa baadhi ya maeneo, wanne kati yao hawapati fursa ya kuanza shule, huku kundi kubwa la wanafunzi likikatisha masomo katika ngazi mbalimbali za elimu.
Hata hivyo imesema inaendelea kuwawezesha watoto, vijana na watu wazima waliokosa fursa ya elimu ndani ya mfumo rasmi kurejea na kuendelea na masomo yao.
Mkuu wa Taasisi hiyo, Profesa Philipo Sanga, amesema katika wakati Wiki ya utumishi wa Umma katika viwanja vya Chinangali Park Mkoani Dodoma.
Amesema majukumu makubwa ya TEWW ni kushughulikia elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi, sekta ambayo imekuwa muhimu katika kuwasaidia wananchi wengi kupata elimu na ujuzi unaohitajika katika maisha na maendeleo ya taifa.
“Katika kila wanafunzi 100, takribani 31 hudondoka na kushindwa kuendelea na masomo kwa ujumla, zaidi ya wanafunzi laki nne kutoka shule za msingi na sekondari hudondoka kila mwaka na kukosa fursa ya kuendelea na elimu.”
Amebainisha kuwa bila uwepo wa Taasis ya Elimu ya Watu Wazima, idadi kubwa ya wananchi wengi wangeshindwa kupata nafasi ya kurejea katika mfumo wa elimu na kufikia malengo yao.
Profesa Sanga, amesema Taasisi hiyo inatekeleza miradi mbalimbali ya elimu ya msingi na sekondari nje ya mfumo rasmi, inayolenga kuwapa wananchi fursa ya kupata elimu, maarifa na ujuzi unaowawezesha kujitegemea na kuchangia maendeleo ya taifa.
Aidha, amesema TEWW kupitia Chuo cha Elimu ya Juu cha Elimu ya Watu Wazima hutoa programu za elimu kuanzia ngazi ya cheti, stashahada, shahada hadi shahada za uzamivu kwa lengo la kuandaa wataalamu wabobevu watakaosaidia maendeleo ya nchi.
Ameongeza kuwa katika kila mkoa kuna viongozi wa elimu ya watu wazima wanaosimamia shughuli za taasisi hiyo na kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi katika maeneo mbalimbali.
Kuhusu elimu ya juu, Profesa Sanga amesema Taasis ya Elimu ya Watu Wazima imefanikiwa kudahili zaidi ya wanafunzi 6,000 na kwamba zaidi ya wanafunzi 2,000 huhitimu kila mwaka, jambo linaloonyesha mchango mkubwa wa taasisi hiyo katika kuboresha sekta ya elimu nchini.

