Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumsihi, Juma Mkomi (kushoto) akifurahia jambo baada ya Meneja Rasilimaliwatu Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Gloria Mboya (katikati mwenye fulana nyeusi) kumpatia maelezo ya huduma zinazotolewa kwenye banda la PSSSF kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwenye viwanja vya Chinangali jijini Dodoma Juni 22, 2026.
Na Mwandishi Wetu
DODOMA: KATIBU Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Juma Mkomi, amepongeza Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwa ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Akitembelea banda la PSSSF Juni 22, 2026, Mkomi amesema mfuko huo umeonyesha jitihada kubwa katika kutoa elimu na huduma mbalimbali kwa wananchi pamoja na wanachama wake.
“Niwapongeze sana kwa ushiriki wenu, lakini pia kwa kutoa elimu na kuhudumia wananchi. Ninaamini katika maonesho haya mmekutana na wanachama wenu wengi. Hongereni sana,” amesema Mkomi.
Akitoa taarifa kwa Katibu Mkuu huyo, Meneja wa Rasilimali Watu wa PSSSF, Gloria Mboya, amesema hadi kufikia alasiri ya Juni 22, wananchi 365 walikuwa wametembelea banda la mfuko huo na kupata huduma mbalimbali.
Amesema wengi wa waliotembelea banda hilo wameunganishwa na huduma za kidijitali kupitia mfumo wa PSSSF Portal, unaowawezesha wanachama kupata huduma kwa urahisi zaidi.
Kupitia simu janja au kompyuta, wanachama wanaweza kuangalia taarifa za michango yao, kuwasilisha na kufuatilia madai mbalimbali, kusasisha taarifa binafsi na za wategemezi wao, huku wastaafu wakipata fursa ya kujihakiki kwa njia ya mtandao.
Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu ya “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu” na yanatarajiwa kufikia kilele chake Juni 23, 2026.

