Na Lucy Lyatuu,Dodoma
MSEMAJI Mkuu wa Serikali,Gerson Msigwa ametumia bonanza la CRDB Bank Grand Bunge 2026 kuhamasisha jamii kukusanyika kwenye masuala yanayohusu michezo na sio yale ya kuvuruga amani ya nchi.
Amesema hayo wakati akizungumza katika bonanza hilo lililofanyika katika uwanja wa Jamhuri na kushirikisha wabunge, mabalozi wanaowakilisha nchi zao pamoja na wadau wa michezo ambao wameonesha umoja na ushirikiano.
Katika bonanza hilo matembezi yameanzia katika viwanja vya Bunge kuelekea uwanja wa Jamhuri yakiongozwa na Naibu Spika Daniel Sillo yakiongozwa pia na kauli mbiu isemayo ” Pamoja AFCON 2027 Tanzania Tupo Tayari.
Akizungumza Msigwa amesema kupitia AFCON Tanzania itanufaika na utalii,biashara,uchumi kukua na kuongeza kuwa mabonanza kama hayo yana umuhimu mkubwakujenga amani na ushirikiano.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela amesema Benki itaendelea kutumia majukwaa ya michezo kuhamasisha afya, mshikamano na maendeleo ya jamii, sambamba na kuimarisha mahusiano na wadau mbalimbali nchini.
Ameeleza kuwa Benki ya CRDB inaendelea kuunga mkono juhudi za Taifa katika maandalizi ya AFCON 2027, ikitambua nafasi ya michezo katika kukuza uchumi, kuimarisha taswira ya nchi na kuleta fursa kwa Watanzania.
Amesisitiza kuwa Benki itaendelea kuwa mshirika wa maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo michezo, kwa lengo la kuchangia ustawi wa Taifa na wananchi kwa ujumla.
Naibu Spika Sillo amesema bonanza linajenga afya na kuipongeza serikali kukubali AFCON kufanyika nchini.

