Na Mwandishi wetu
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni amelikabidhi Jeshi la Polisi magari 77 kwa ajili kurahisha utekelezaji wa majukumu yake ya kusimamia usalama wa raia na mali zao.

hatua hiyo ni mwendelezo wa jitihada za Serikali kulifanya Jeshi hilo kuwa la kisasa lenye vifaa, na weledi wa kuzuia uhalifu.
Akikabidhi magari hayo, Waziri Masauni amelitaka Jeshi hilo kuhakikisha linayatumia vyema magari hayo kwa kupunguza malalamiko ya wananchi ikiwa ni sambamba na kuyatunza ili kuthamini jitihada zinazofanywa na Serikali.
Naye Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP),. Camillus Wambura ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuliwezesha Jeshi hilo kuwa la kisasa.

Amesema hivyo ni wajibu Polisi kuhakikisha uhalifu unaendelea kupungua huku akiwaasa madereva wa magari hayo kuzingatia sheria za usalama barabarani ili magari hayo yaweze kudumu.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge, Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama, Vita Kawawa ametoa rai kwa madereva wa magari hayo kupatiwa mafunzo, huku Mkurugenzi wa Kampuni ya Kifaru Motors, Brigedia Jenerali Mstaafu Michael Luwongo akiahidi kuwa kampuni yake imejiandaa kulisaidia Jeshi hilo msaada kitaalamu, ushauri na kiufundi pale itakapohitajika.
