Na Lucy Lyatuu,Dodoma
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba
amezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha zinaondoa urasimu katika kuanzisha biashara mpya au viwanda vipya katika maeneo yao.
Amesema kwa kufanya hivyo, kutasaidia kuchochea upatikanaji wa ajira mpya kwa vijana, kukuza kipato kwa wawekezaji na wafanyabiashara pamoja na kukuza pato la Taifa.

Kadhalika amezitaka mamlaka hizo kuweka mikakati ya kushughulikia changamoto mbalimbali zikiwemo za tozo zisizo rafiki kwa sekta binafsi.
Dkt Nchemba amesema hayo katika
wakati akifunga Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (Mkumbi II) uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage, HAZINA, jijini hapa.
Akizungumza amewataka Wakuu wa Mikoa na watendaji wao katika mikoa yote nchini kujipanga kutoa taarifa kuhusu uwekezaji na ukuzaji wa biashara kwenye mikoa yao kila wanapotoa taarifa kwa viongozi wa kitaifa.

“ Ni muhimu Kwa nafasi zenu Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala na Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha mnabeba jukumu la kuwa mabalozi wa uwekezaji katika maeneo yenu kwa kutambua na kutangaza fursa mbalimbali zilizopo katika maeneo mliyopo,” amesema.
Amesema Kila Kiongozi wa mkoa aahakikishe anapotoa taarifa aeleze ameongeza uwekezaji kwa kiasi gani, amekuza biashara kwa kiwango gani na katika kuongeza biashara mpya
Amesema mapendekezo yote yaliyowasilishwa na washiriki wa mkutano huo ambao ni Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Wakurugenzi yaandaliwe katika mfumo wa mkakati wa utekelezaji ili kuwezesha utekelezaji wake kwa ufanisi.
Amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alishasema isiwepo sheria inayoleta kikwazo katika utendaji kazi wa serikali. Haya tuliyoyabaini, tuyaweke kwenye majedwali na kubainisha lipi ni kikwazo na lipi limefanyika. Leteni hayo mapendekezo.”
“Kuhusu suala la utitiri wa taasisi za udhibiti na kodi, andaeni mapendekezo mahsusi na yawasilishwe kwa Waziri wa Fedha ili yaweze kuingizwa katika Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka huu. Hatua hii inalenga kuwa sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini,” amesema

Awali Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo amewashukuru Wakuu wa Mikoa yote kwa ushirikiano wao na jinsi walivyolipa kipaumbele suala la uwekezaji kwenye maeneo yao.
Amesema ofisi yake kwa kushirikiana na Waziri wa Nchi, OWM – TAMISEMI wanaandaa nyenzo za kushindanisha mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kuvutia uwekezaji na kulinda biashara.
Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar amewaeleza washiriki wa mkutano huo kwamba matarajio ya Serikali kwenye utekelezaji wa DIRA 2050 unaendana na MKUMBI II kwenye maeneo yao.
Amesema Uchumi wa Tanzania kwa sasa ni dola za Marekani bilioni 100 ikichanganywa na uzalishaji wa bidhaa zote, huduma na biashara za ndani na za nje .
” Katika miaka 25 ijayo, tunataka tufikie dola za Marekani trilioni moja, maana yake tukue zaidi ya mara 10.” amesema.

