Na Mwandishi Wetu
NJOMBE: ZAIDI ya makampuni 100, yakiwemo ya uchimbaji wa madini, yanatarajiwa kushiriki maonesho ya Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) yatakayofanyika katika viwanja vya Sabasaba, mjini Njombe.
Maonesho hayo yatafunguliwa rasmi Aprili 24 na kufikia kilele chake Aprili 29, mwaka huu 2026 ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi Duniani pamoja na shamrashamra za Mei Mosi.
Akizungumza na waandishi wa habari wa Chama cha Waandishi wa Habari na Wafanyakazi wa Vyombo vya Habari Tanzania (JOWUTA), Meneja wa OSHA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Wilbert Ngowi, amesema maandalizi yote yamekamilika.
Amesema pamoja na maonesho hayo, kutakuwa na utoaji wa tuzo kwa makampuni na taasisi zitakazofanya vizuri katika kuzingatia masuala ya usalama na afya kazini.
“Tunatarajia tuzo hizi zitatolewa Aprili 29 katika ukumbi wa Agrimet mjini Njombe, ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Ajira na Mahusiano ya Kazi, Deus Sangu,” amesema Ngowi.
Aidha, OSHA imeandaa semina kwa wafanyakazi Aprili 27 zitakazojikita katika masuala ya kazi, afya na saikolojia, sambamba na michezo mbalimbali itakayofanyika katika kipindi chote cha maadhimisho hayo.
Ngowi amesema wamejipanga kuhakikisha maadhimisho ya Mei Mosi mwaka huu yanafanikiwa, huku akitoa wito kwa makampuni ambayo bado hayajakamilisha usajili kujitokeza mapema kupitia mfumo wa OSHA.
Kwa upande wake, JOWUTA imethibitisha kushiriki kwa mara ya kwanza katika maadhimisho ya Mei Mosi kitaifa mwaka huu 2026 mkoani Njombe pamoja na baadhi ya mikoa mingine nchini.

