WAZIRI wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omari, amesisitiza umuhimu wa kuwaunganisha wazalishaji na masoko pamoja na kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa nchini zinafikia viwango vinavyotakiwa pamoja kuzitangaza ili zifahamike na kupata masoko.
Aidha amewataka , wadau kuongeza juhudi za kutangaza bidhaa za ndani na kuchagiza kuwa uzalishaji wenye tija hauwezi kuwa na maana endapo bidhaa hazitafika sokoni kwa ubora, kiasi na wakati unaohitajika.
Khamis amesema hayo katika ziara yake katika Maonesho ya Nane Nane jijini Dodoma, ambapo ametembelea mabanda mbalimbali
yanayohusisha wadau wa kilimo, mifugo, uvuvi na sekta zinazohusiana na uzalishaji, akisisitiza umuhimu wa Serikali kuweka nguvu pamoja kuanzia uzalishaji, usindikaji, upatikanaji wa mitaji hadi masoko.
Akiwa katika maonesho haho, amezitaka wizara na taasisi za Serikali kuacha kufanya kazi kwa mtazamo wa kila sekta kivyake na badala yake kuunganisha nguvu katika kuongeza uzalishaji wa kilimo, mifugo na uvuvi, akisema ushirikiano huo ni muhimu katika kuongeza tija na kukuza uchumi wa Taifa.
Amesema wizara zinazohusika na fedha, kilimo, mifugo, uvuvi na viwanda zinapaswa kufanya kazi kwa mtazamo mmoja ili kutatua changamoto zinazowakabili wazalishaji, huku akisisitiza umuhimu wa kuwekeza katika utafiti utakaosaidia kubaini vikwazo vya uzalishaji na kupata suluhisho zenye uwezo wa kuongeza tija.
“Mbali ya kusema niko kwenye kilimo, niko kwenye fedha, mimi niko viwanda, tunahitaji kwenye maendeleo ya uzalishaji katika sekta ya kilimo, pamoja na mchakato wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi, pamoja na huduma ambazo zinaambatana na hili,” amesema Khamis.
Kuhusu sekta ya uvuvi, Waziri huyo amesema Serikali inapaswa kuendelea kuunga mkono ufugaji wa samaki kutokana na umuhimu wake katika kuongeza upatikanaji wa chakula chenye protini, akibainisha kuwa changamoto zinazoikabili sekta ya uvuvi wa asili katika bahari na maziwa zinaifanya Tanzania kuhitaji kuongeza uzalishaji kupitia njia mbadala.