Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: WAFANYABIASHARA ndogo ndogo wametakiwa kuchangamkia fursa ya mkopo wa serikali wenye masharti nafuu na riba ya asilimia saba kupitia Benki ya NMB.
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu ametoa rai hiyo alipozindua taarifa ya Utafiti kuhusu Waendesha Pikipiki Wanawake mkoani Dar es Salaam.

Mdemu amesema tayari serikali imetoa Sh. Bilioni nane kwa ajili ya kutoa mikopo hiyo.
” Mikopo hiyo inalenga kuimarisha uchumi wa wafanyabiashara ndogo ndogo ili waweze kukuza mitaji na kuboresha mazingira ya biashara.
” Muhimu kuelewa kuwa ili uweze kupata mkopo huo, sharti usajiliwe kwenye mfumo na kupatiwa kitambulisho cha kidijitali, ambacho kinakuwezesha kupata mkopo. Hivyo nendeni mjiandikishe kwenye Halmashauri kwa Maofisa Maendeleo ya Jamii,” amesema.
Amesema lengo la serikali ni kuhakikisha inaweka mazingira wezeshi na rafiki ili wafanyabiashara ndogo ndogo waweze kunufaika na fursa za kiuchumi na kijamii ikiwemo mikopo ya biashara kupitia taasisi za fedha.

Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Mawasiliano na Uchukuzi Tanzania (COTWU – T), Juliana Mpanduji amesema usafirishaji ni nguzo muhimu kwa uchumi wa taifa na tegemeo la uchumi wa dunia.