Na Lucy Lyatuu, Dodoma
TAASISI Ya Kimataifa Ya Kielektroniki Inajojihusisha Na Utafiti Wa Mazao Mbalimbali (IITA) kwa kushirikiana na Taasisi Ya Utafiti Wa Kilimo Tanzania (TARI) imegundua teknolojia ya kisasa ya kuharakisha uzalishaji wa mbegu bora za zao la muhogo kwa muda.mfupi,jambo linalowezesha upatikanaji wa.mbegu kwa wakulima.
Teknolojia hizo ni Single Node Cutting, ambapo sehemu yenye jicho moja ya mmea wa muhogo hukatwa na kupandwa katika kontena au moja kwa moja kwenye udongo, kisha hupewa maji na matunzo stahiki.
Mtafiti kutoka IITA, Betha Lasway, amesema hayo wakati akizungumza katika maonesho ya Nanenane jijini Dodoma na kuongeza kuwa uzalishaji wa mbegu bora huanzia katika utafiti wa awali na maabara, ambako watafiti huhakikisha mimea inayozalishwa inakidhi viwango vya ubora na usafi wa juu kabla ya kupelekwa katika hatua za breeding kwa ajili ya uchunguzi na uzalishaji zaidi.

Amesema teknolojia hizo zinawawezesha kuzalisha mbegu za muhogo ambazo mkulima anaweza kutumia kulingana na muda wa aina husika, kuanzia miezi tisa hadi 18.
Amesema katika teknolojia hizo ni Single Node Cutting, kipando cha muhogo hukatwa na kupandwa katika kontena au moja kwa moja kwenye udongo, kisha hupewa maji na matunzo stahiki.
Amesema kwa kutumia teknolojia hiyo, watafiti wanaweza kuzalisha hadi mimea 700 kwa mwaka, ikilinganishwa na takribani mimea 25 inayoweza kupatikana kwa njia ya kawaida ya uzalishaji wa miche kwa kipindi hicho.
Betha amesema teknolojia nyingine ni kutumia sehemu ya juu yenye majani ya mmea na kuiotesha katika mfumo maalumu wa maji, ambapo maji hubadilishwa kila siku ili kuwezesha mizizi kuota.
Kwa mujibu wake, mizizi huanza kuonekana ndani ya siku saba na kuenea vizuri ndani ya siku 14, baada ya hapo miche huhamishiwa kwenye udongo na ndani ya takribani miezi miwili huwa tayari kupelekwa shambani.
Ameeleza kuwa teknolojia hizo zinawezesha uzalishaji wa idadi kubwa ya mbegu kwa muda mfupi na hivyo kusaidia kuhakikisha wakulima hawakabiliwi na uhaba wa mbegu bora.
Aidha, amesema Machi 2026, IITA kwa kushirikiana na TARI iliongeza aina mbili mpya za mbegu bora za muhogo zilizoidhinishwa, ambazo ni Kimbilio na Kipato, na kufanya idadi ya aina za mbegu bora za muhogo zilizoidhinishwa kufikia 27 kutoka 25.
Amesema aina hizo zina uwezo wa kustahimili ukame, wadudu na magonjwa, huku aina ya Kipato ikiwa na uwezo mkubwa wa uzalishaji unaoweza kufikia tani 62 kwa hekta, pamoja na kuwa na kiwango kizuri cha wanga.
Katika hatua nyingine amewataka wakulima kuacha kutumia mbegu za muhogo za kienyeji zisizo na uhakika wa afya, akisema baadhi yake huathiriwa na magonjwa ya virusi ambayo yanaweza kusababisha hasara kubwa kwa mkulima, huku hakuna dawa ya moja kwa moja ya kutibu mimea iliyoathirika.
Amesema hatua zinazochukuliwa ni kung’oa, kuchoma au kuzika mimea iliyoathirika, hivyo amewashauri wakulima kutumia mbegu bora zinazopatikana katika vituo vya TARI.
Kadhalika amewataka kuongeza thamani ya muhogo kwa kutumia unga wake kutengeneza bidhaa kama mikate, keki na biskuti, hatua inayoweza kuongeza fursa za soko na kipato kwa wakulima.

