Na Lucy Lyatuu, Dodoma
SHIRIKA La Mawasiliano Tanzania (TTCL) limesema linatumia maonesho ya Nanenane kuelimisha kuhusu huduma ya uhifadhi wa taarifa kidijitali (Cloud Service) inayotolewa kupitia Kituo cha Taifa cha Data, kwa lengo la kurahisisha uhifadhi na matumizi salama ya taarifa.
TTCL imewataka Watanzania, wakiwemo wafanyabiashara, wanafunzi, waandishi wa habari na taasisi mbalimbali kutumia huduma hiyo.
Ofisa Tehama wa TTCL, Alfred Thawe, amesema huduma hiyo imeanzishwa ili kuwawezesha Watanzania kuhifadhi data na mifumo yao ndani ya miundombinu iliyopo nchini, bila kulazimika kutegemea huduma za nje ya Tanzania.
Amesema kupitia maonesho hayo wanahimiza wananchi kujifunza kuhusu huduma hiyo huduma hiyo ambayo inaweza kutumiwa na makundi mbalimbali.
Ameyataja makundi hayo kuwa ni pamoja na wanafunzi wanaofanya tafiti, wajasiriamali wanaohitaji kuhifadhi taarifa za biashara zao pamoja na taasisi zenye mifumo inayohitaji miundombinu ya kuhifadhi na kuendesha taarifa.
Kadhalika amesema, kituo hicho kinatoa huduma za miundombinu ya TEHAMA pamoja na huduma nyingine zinazohusiana na uhifadhi wa data.
” TTCL pia inatoa fursa kwa waandishi wa habari na wafanyabiashara wadogo na wa kati wanaohitaji kusajili na kutumia majina ya tovuti , huku akisisitiza kuwa huduma hizo zinapatikana kwa gharama nafuu,”amesema.
Thawe amesema moja ya faida kubwa ya kutumia miundombinu hiyo ni kuhakikisha taarifa za Watanzania zinahifadhiwa ndani ya nchi, jambo linaloongeza udhibiti na upatikanaji wa data hizo.

