VETA Dodoma Yatengeneza Biskuti Za Uwele, Yahamasisha Vijana Kujiunga Kupata Mafunzo
Na Lucy Lyatuu,Dodoma
MAMLAKA Ya Elimu Na Mafunzo Ya Ufundi Stadi (VETA), Dodoma inahimiza wananchi hususani vijana kujiunga na Mamlaka hiyo ili kujifunza namna ya kutumia mazao yanayopatikana kwenye maeneo wanauoishi na kutengeneza bidhaa tofautitofauti zenye kuwapatia kipato.
Mwalimu wa Chuo cha VETA Dodoma,Amina Juma amesema hayo wakati akizungumza katika maoneshonya Nanenane jijini humo na kuongeza kuwa Mamlaka hiyo imeweza kutumia uwele kutengeneza biskuti na keki ambazo kiafya zina manufaa.
Kuhusu manufaa kwa bidhaa za uwele amesema wametumia zao hilo kutengeneza bidhaa hizo kuonesha jinsi lilivyo na faida kwenye mwili wa binadamu kwa kuimarisha mifupa na hata viungo kwa ujumla.
” Uwele unaimarisha afya ya mwili kwa watoto na wazee na hata kupunguza homa za mifupa,” amesema Amina na kuwataka wananchi kufika katika banda la VETA ili kupata elimu na manufaa ya zao hilo ambalo hupatikanankwa wingi mkoani humo.
Amesema pia uwele husaidia kuimarisha afya ya moyo kwa kuwa ndani yake kuna madini ya potasium na magneziam kwa wingi ambapo huwasaidia kupata ahueni na pia kusaidia wenye kisukari pia kupata nafuu kuyokana na chakula kuchakatwa vyema mwilini.
Amina ameongeza kuwa uwele ni zao linalopatikana kwa wingi na wameamua kulitumia kutengeneza bidhaa hizo ambazo pia zina manufaa kwa mwili wa binadamu.
Mbali na zao hilo,Amina amesema chini ya kitengo cha uhudumu wa chakula na vinywaji ndani ya Idara ya Hotel Menejimenti katika Mamlaka hiyo hufundisha vijana namna ya kujiajiri katika kitengo hicho.
Amesema wamekuwa wakifundisha vijana kujiandaa na soko la hotel wakitoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu wakifundisha namna ya kutumia mazao yanayoweza kutengeneza bidhaa mbalimbali,kuongezea thamani ya mazao na kuwataka vijana kujiunga na mafunzo hayo.

