Na Lucy Ngowi
DODOMA: MAMLAKA ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) imeendelea kuhamasisha matumizi sahihi ya viuatilifu kwa wakulima na wafanyabiashara, ikieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuongeza uzalishaji wa mazao na kulinda afya ya binadamu pamoja na mazingira.
Akizungumza katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, Mkaguzi wa Biashara ya Viuatilifu wa TPHPA, Ereneus Mwinuka, amesema wakulima wengi bado wanakabiliwa na changamoto ya kutotambua viuatilifu vinavyofaa kwa ajili ya kudhibiti wadudu na magonjwa yanayoshambulia mazao yao.
Amesema mamlaka hiyo inatumia maonesho hayo kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kusoma taarifa zilizopo kwenye lebo za viuatilifu kabla ya matumizi, ili kuhakikisha wanachagua bidhaa sahihi kulingana na aina ya kisumbufu wanachotaka kudhibiti.
Kwa mujibu wa Mwinuka, matumizi ya viuatilifu visivyofaa yanaweza kusababisha hasara kwa mkulima kutokana na kushindwa kudhibiti tatizo husika, hivyo ni muhimu kutambua kwanza kisumbufu kabla ya kufanya ununuzi wa bidhaa.
Aidha, amewataka wakulima kuhakikisha wanatumia viuatilifu vilivyosajiliwa na kuthibitishwa na TPHPA kwa kuangalia namba za usajili pamoja na tarehe ya mwisho wa matumizi ili kuepuka matumizi ya bidhaa zisizo salama au zisizo na ufanisi.
Mbali na wakulima, TPHPA pia imekuwa ikitoa elimu kwa wafanyabiashara wa viuatilifu kuhusu taratibu za biashara hiyo, ikiwemo masharti ya kupata leseni na wajibu wao wa kuwapa wakulima ushauri sahihi kuhusu matumizi ya bidhaa wanazouza.
Mwinuka amesema mwitikio wa wananchi kutembelea banda la mamlaka hiyo umekuwa mkubwa, jambo linaloonyesha kuongezeka kwa uelewa na hamasa ya kutafuta taarifa sahihi kuhusu matumizi ya viuatilifu.
Ameeleza kuwa wageni wengi waliotembelea banda hilo wamepata maarifa mapya yatakayowasaidia kufanya maamuzi bora wakati wa kununua na kutumia viuatilifu katika shughuli za kilimo.

