Na Lucy Ngowi
DODOMA: WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, ametembelea banda la Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, ambapo alijionea kazi za ubunifu zinazofanywa na wahitimu wa taasisi hiyo, ikiwemo michoro ya ramani za majengo iliyobuniwa na mhitimu mwenye ulemavu wa mikono.
Akiwa katika banda hilo, Meneja wa Kampuni Tanzu ya VETA, Marco Kapinga, amesema VETA inaendelea kutoa fursa za mafunzo kwa vijana wenye mahitaji maalum na kuwawezesha kujitegemea kupitia ujuzi wanaoupata.
Amemtambulisha Mhitimu wa VETA Dodoma, Joseph Mtei, katika fani ya uchoraji wa ramani za majengo, ambaye kwa sasa ameajiriwa na kampuni hiyo baada ya kuonyesha umahiri mkubwa katika taaluma yake.

“Joseph alipata mafunzo VETA na sasa ni sehemu ya timu yetu. Kupitia ujuzi wake, amekuwa akibuni michoro mbalimbali ya majengo na kushiriki katika uzalishaji wa huduma zinazotolewa na kampuni,” amesema Kapinga.
Kwa upande wake, Mtei amesema michoro yote ya ramani za majengo iliyooneshwa katika banda hilo imebuniwa na yeye na tayari baadhi yake imetekelezwa katika miradi mbalimbali.

“Ramani zote mnazoziona hapa nimezichora mimi mwenyewe. Nimezitengeneza kwa kutumia ujuzi nilioupata VETA, na nyingi kati ya hizo tayari zinatekelezwa,” amesema.

