Na Lucy Lyatuu, Dodoma
WIZARA ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imesema imetenga sh bilioni 30 Kwa ajili ya kulipa fidia Kwa maeneo yote ya wananchi,fedha ambayo italipwa ndani ya bajeti ya Wizara hiyo 2026/2027.
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt Rhimo Nyansaho amesema hayo bungeni wakati akihitimisha hotuba ya bajeti yake.
Katika bajeti hiyo,Wizara inaomba kuidhinishiwa Sh trilioni 4.28 kwa mwaka wa fedha 2026/27 kwa ajili ya kutekeleza vipaumbele mbalimbali ikiwemo kuimarisha ulinzi wa taifa, teknolojia za kijeshi na kuongeza uwezo wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Kuhusu fidia amesema fedha hizo zitalipwa na hazina katika kipindi hicho Cha bajeti na kwamba wananchi wamekuwa welewa wasio na vurugu hata pale maeneo yao yanachukuliwa na Jeshi.

Amewataka Wananchi kuwa sehemu ya kuzuia migogoro na zaidi kuwa na mapenzi na uzalendo na nchi yao.
Akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo, amesema kati ya fedha hizo, Sh trilioni 3.85 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh bilioni 426.5 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Dkt. Nyansaho alisema katika mwaka wa fedha 2026/27 wizara hiyo itatekeleza mpango na bajeti yake kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano wa 2026/27 hadi 2030/31, Malengo ya Maendeleo Endelevu 2030 (SDGs), pamoja na mpango mkakati wa wizara na taasisi zake.
Amesema vipaumbele vya wizara hiyo vitajikita katika maeneo nane, yakiwemo kuimarisha jeshi kwa zana na vifaa vya kisasa vya kijeshi, teknolojia ya mawasiliano pamoja na rasilimali watu.
Kuhusu mafunzo ya JKT amesema Katika kuhakikisha wahitimu wote wa Kidato cha Sita wanapata fursa ya kujiunga na mafunzo ya JKT, wizara imeendelea kuboresha miundombinu ya kambi ambapo kwa mwaka wa fedha 2025/26 vijana 60,000 walichukuliwa kw aajili ya kujiunga na JKT

Amesema Serikali inaendelea kufungua kambi mpya na kuboresha zilizopo ili kuwezesha JKT kuchukua vijana 140,000 ifikapo mwaka 2031, hatua itakayowezesha wahitimu wote wa Kidato cha Sita kupata nafasi ya mafunzo.
“Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea vijana uzalendo, ukakamavu, umoja wa kitaifa na kuwapatia stadi za kazi na maisha ili waweze kujitegemea wanaporejea uraiani,” amesema.
Aidha, Serikali inapanga kuboresha mfumo wa mafunzo hayo kwa kuingiza zaidi elimu ya ufundi, kwakuwa sio kila kijana anayepitia JKT analenga kujiunga na vyombo vya ulinzi na usalama.

