Na Mwandishi Wetu
NJOMBE: RAIS Dkt. Samia Suluhu Hassan amemtunuku tuzo ya Mfanyakazi Hodari Mkurugenzi wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Profesa Joseph Ndunguru, katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe.
Profesa Ndunguru, anayewakilisha Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia na Taasisi za Utafiti (RAAWU), alijiunga na TPHPA mwaka 2023 na kuongoza mageuzi makubwa yaliyoifanya taasisi hiyo kuwa mfano barani Afrika.
Mafanikio hayo ni pamoja na kuboresha maabara na kuongeza uwezo wa uchambuzi wa viuatilifu, pamoja na kuunganisha ofisi 47 za mipakani katika mfumo mmoja.

Hatua hiyo imeongeza ufanisi na mapato kutoka Sh. Bilioni 14 mwaka 2023 hadi bilioni 69 ndani ya miezi minane (Julai 2025–Februari 2026).
Akizungumza katika sherehe hizo, Rais Samia aliwapongeza wafanyakazi wote kwa mchango wao katika kukuza uchumi na kuahidi kuendelea kuboresha maslahi yao.
“Serikali inatambua mchango wenu na itaendelea kuboresha maslahi pamoja na kulipa madai na kutafuta ajira zenye staha,” amesema.

Kwa upande wake, Profesa Ndunguru amesema ushindi huo unatokana na ushirikiano wa wafanyakazi na uongozi wa Serikali.
Ameeleza kuwa TPHPA sasa inawezesha vipimo vya ubora wa mazao kufanyika ndani ya nchi, hivyo kupunguza gharama na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa.
Ameongeza kuwa mamlaka hiyo imeanza kutafuta masoko ya kimataifa kwa mazao ya kimkakati, ikiwemo kuwasaidia wazalishaji wa parachichi na viazi kupata soko nchini China.
Pia, mipango inaendelea ya kujenga maabara mpya Arusha na Makambako pamoja na kituo cha kuhifadhi mbegu za asili 10,000.
Aidha, amesema TPHPA itaendelea kushirikiana na wanahabari kupitia JOWUTA kuelimisha umma na kudhibiti uingizaji wa viuatilifu visivyoidhinishwa.

Profesa Ndunguru akiwa na washindi wa tuzo hodari kitaifa wa Chama cha Wafanyakazi Katika Vyombo vya Habari (JOWUTA), Idda Mushi na Lucy Ngowi
Profesa Ndunguru pia ameahidi kufanyakazi na chama cha wafanyakazi katika vyombo vya Habari nchini(JOWUTA) kwa kuwajengea uwezo wanahabari juu ya kazi za Mamlaka hiyo.
Mwenyekiti wa JOWUTA Taifa, Mussa Juma amempongeza Profesa Ndunguru na wafanyakazi wote wa TPHPA Kwa kazi nzuri wanayofanya na pia ameshukuru TPHPA kuwa mmoja wa wafadhili wa zawadi za waandishi hodari mwaka 2026.

