Na Mwandishi Wetu,
DODOMA: MFUKO wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umeendelea kuimarika kwa kasi, ukifikia thamani ya Sh Trilioni 11.2 hadi Machi 2026 kutoka Trilioni 4.3 mwaka 2020, hatua inayoonesha ukuaji wa uwekezaji, uimara wa usimamizi na ongezeko la wanachama kupitia Hifadhi Skimu.
Akizungumza jijini Dodoma April 27, 2026 wakati akifungua Mkutano wa 56 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NSSF, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, amesema mafanikio hayo yametokana na mageuzi ya usimamizi, uwekezaji wenye tija na matumizi ya teknolojia.

Amesisitiza kuwa Hifadhi Skimu ni nguzo muhimu ya mustakabali wa hifadhi ya jamii nchini, akibainisha kuwa Serikali inalenga kuwafikia Watanzania wengi zaidi, hususan waliojiajiri.
“Upanuzi wa hifadhi skimu ni hatua muhimu ya kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nje ya mfumo wa hifadhi ya jamii,” amesema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Masha Mshomba, amesema Mfuko unalenga kufikia thamani ya Sh. Trilioni 24.7 ifikapo Juni 2031 na kuongeza wanachama hadi milioni 6.6, huku ukiimarisha matumizi ya TEHAMA kufikia asilimia 99 ya huduma.

Ameeleza kuwa mafanikio hayo pia yametokana na utawala bora na uwazi uliowezesha NSSF kupata hati safi ya ukaguzi. Hata hivyo, alibainisha changamoto za baadhi ya waajiri kuchelewesha michango na uelewa mdogo wa hifadhi ya jamii.
Waziri Sangu aliipongeza NSSF kwa uwekezaji katika miradi kama kiwanda cha sukari cha Mkulazi, akisema inachochea ajira na uchumi.
Ameongeza kuwa mipango ya Mfuko inaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, inayolenga asilimia 70 ya Watanzania kufikiwa na hifadhi ya jamii.


