Na Mwandishi Wetu,
DODOMA: SERIKALI imesema imejipanga kikamilifu kuhakikisha maandalizi ya mashindano ya AFCON 2027 yanaenda sambamba na uboreshaji wa miundombinu muhimu nchini.
Kauli hiyo imetolewa jijini Dodoma na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, kutokana na hoja za wabunge kuhusu hali ya miundombinu kuelekea mashindano hayo makubwa ya soka barani Afrika.
Makonda amesema tayari serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ikiwemo viwanja vya michezo, barabara na huduma nyingine muhimu ili kufikia viwango vinavyotakiwa kimataifa.
Ameeleza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unaendelea kwa kasi, huku serikali ikihakikisha Tanzania inajiandaa kuwa mwenyeji bora wa mashindano hayo, pamoja na kutumia fursa hiyo kukuza sekta za michezo na utalii.
Katika hatua nyingine, Makonda amegusia maendeleo ya tasnia ya urembo nchini, akisema imeendelea kukua kutokana na kuongezeka kwa makampuni yanayoandaa mashindano ya urembo.
Amebainisha kuwa hali hiyo imekuwa chachu ya kukuza vipaji na ajira kwa vijana, huku ushindani unaojitokeza ukichangia kuboresha ubora wa mashindano na kuifikisha tasnia hiyo katika viwango vya kimataifa.

