Na Mwandishi Wetu
PRETORIA, AFRIKA KUSINI: MKUTANO wa siku mbili wa Baraza la Mawaziri wa jumuiya ya kikanda ya nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) umehitimishwa jijini Pretoria nchini Afrika Kusini Machi 13, 2026.
Mkutano huo ulilenga kuongeza kasi ya mtangamano wa kikanda ili kuharakisha maendeleo, kutengeneza ajira, kuimarisha usalama wa chakula na kuongeza upatikanaji wa nishati kwa wananchi wa nchi wanachama.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ngwaru Maghembe, akifuatana na Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula.
Akizungumza wakati wa kufunga mkutano huo, Mwenyekiti wa mkutano ambaye pia ni Waziri wa Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano wa Afrika Kusini, Ronald Lamola, amesisitiza umuhimu wa nchi wanachama kudumisha umoja na mshikamano ili kuhakikisha maazimio yote yaliyokubaliwa yanatekelezwa kikamilifu.

Katika majadiliano yao, Mawaziri wamesisitiza umuhimu wa kuharakisha utekelezaji wa miradi ya kikanda, hususan ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji, matumizi ya nishati safi na kuongeza uwekezaji katika sekta ya viwanda.
Aidha, mkutano huo ulijadili utekelezaji wa bajeti ya SADC kwa mwaka wa fedha 2025/2026 na maandalizi ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027.

Wakati wa mkutano huo, nchi wanachama pia zilitahadharishwa kuhusu kuongezeka kwa taharuki katika siasa za kimataifa pamoja na vita vinavyoendelea katika Mashariki ya Kati, hali inayoweza kuathiri uchumi wa nchi za SADC na dunia kwa ujumla.
Mkutano huo ulitanguliwa na vikao vya Kamati ya Makatibu Wakuu pamoja na Kamati ya Fedha, ambavyo vilikuwa na jukumu la kuandaa ajenda na kuwasilisha ripoti mbalimbali za utekelezaji kwa ajili ya majadiliano ya Mawaziri.


