Na Lucy Ngowi
DODOMA: RAIS wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Tumaini Nyamhokya, amesema kuwa shirikisho hilo lipo mstari wa mbele kusimamia haki na maslahi ya wafanyakazi nchini.
Nyamhokya, ambaye pia ni Mwenyekiti Taifa wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU), amesema hayo leo Machi 7, 2026 wakati wa kongamano la wafanyakazi wanawake Tanzania lililoandaliwa na TUCTA.

Akizungumza katika kongamano hilo, Nyamhokya amesema mkombozi wa mwanamke ni mwanamke mwenyewe, hivyo amewataka wanawake kupendana na kushirikiana, huku wakitofautisha masuala ya mtaani na yale ya kazini.
“Mwenzako kama ni mzuri kazini, mtumie na mshirikishe. Kina mama pendaneni. Pia msisahau kwamba mnapokuwa kazini mnakuwa na fursa za ajira, hivyo jiendelezeni zaidi,” amesema.

Aidha, amesema kauli mbiu ya kongamano hilo inahimiza haki na usawa kwa mwanamke na msichana, akisisitiza umuhimu wa kuwalinda wasichana wanaoanza ajira mpya.
Nyamhokya ameongeza kuwa kuna taasisi nyingi zinazosaidia kuwawezesha wanawake kiuchumi, hivyo amewahimiza wanawake kuzitumia fursa hizo ili kujiimarisha zaidi kiuchumi.
“Niwasisitize wanawake kusimama imara na kuwa macho katika kutetea haki zao pamoja na kujiletea maendeleo,” amesema.

