Lucy Ngowi
DODOMA: SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha utendaji wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) ili kuhakikisha sekta ya afya ya mimea inalindwa kwa ufanisi na kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao nchini.
Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde, alisema hayo jijini Dodoma wakati akimwakilisha Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Afya ya Mimea yaliyofanyika viwanja vya NaneNane Nzuguni.

Akizungumza katika maadhimisho hayo yenye kaulimbiu ya ‘Ulinzi wa Bayoanuai ya Mimea kwa Usalama wa Chakula na Lishe’, Silinde alisema afya ya mimea ni msingi muhimu wa usalama wa chakula, lishe bora, ajira na ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya kilimo.
Alisema Serikali inalenga kuimarisha ushirikiano wa taasisi mbalimbali katika kusimamia afya ya mimea, mazingira, wanyama na binadamu ili kukabiliana na changamoto za visumbufu vya mazao zinazoongezeka duniani.
“Changamoto za afya ya mimea haziwezi kutatuliwa na nchi au taasisi moja pekee, hivyo ushirikiano wa pamoja unahitajika ili kulinda uzalishaji wa mazao na mazingira,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA, Joseph Ndunguru, alisema mamlaka hiyo imefanikiwa kudhibiti visumbufu mbalimbali vya mazao nchini, hatua iliyochangia kuimarika kwa usalama wa chakula.
Alisema katika mwaka 2024/2025 Tanzania ilifikia utoshelevu wa chakula kwa asilimia 130 baada ya kuzalisha tani zaidi ya milioni 23 za mazao ya chakula.
Profesa Ndunguru alisema TPHPA imefanikiwa kudhibiti baa la panya katika mikoa 19, kudhibiti ndege waharibifu aina ya kwelea kwelea zaidi ya milioni 231, viwavijeshi katika hekta 219,411 pamoja na nzige waliovamia maeneo mbalimbali nchini.
Aidha alisema mamlaka hiyo imeendelea kufuatilia matumizi ya viuatilifu, kudhibiti magugu vamizi katika Ziwa Victoria na kufanya uchunguzi wa masalia ya viuatilifu kwenye mazao ya chakula ili kulinda afya za walaji na mazingira.


