Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeeleza kuimarisha jitihada za kufufua viwanda vilivyokwama uzalishaji ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi, hususan katika Manispaa ya Musoma mkoani Mara.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amesema hatua hiyo inakuja kutokana na tathmini pamoja na mazungumzo yaliyofanyika kati ya Serikali na wawekezaji kuhusu hatima ya viwanda vilivyokuwa vimesimama kwa muda mrefu.
Amebainisha kuwa makubaliano yamefikiwa kurejesha Kiwanda cha MUTEX kwa mwekezaji wa awali kwa masharti mapya, huku mkataba ukiwa tayari umefanyiwa uhakiki na Mwanasheria Mkuu wa Serikali na kuwasilishwa kwa Msajili wa Hazina kwa hatua zaidi.
Kwa mujibu wa Londo, maboresho ya mwisho ya mkataba huo yanaendelea kukamilishwa kabla ya kukabidhiwa rasmi kwa mwekezaji ili aanze uzalishaji bila kuchelewa.
Kuhusu Kiwanda cha Musoma Dairy, amesema mwekezaji wa awali ameonyesha nia ya kurejea kuendesha shughuli za uzalishaji, na kwamba Serikali inaendelea kupitia ombi hilo kabla ya kufikia uamuzi.
Amekiri kuwa kwa sasa viwanda vya MUTEX na Musoma Dairy havifanyi kazi, jambo linalopunguza fursa za ajira kwa wakazi wa eneo hilo, lakini akasisitiza kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha vinafufuliwa haraka kwa manufaa ya wananchi.
Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Musoma Mjini, Mgore Kigera, Londo ameuliza kama mchakato wa mkataba mpya unaweka masharti yatakayomhakikishia mwekezaji kuanza uzalishaji kwa wakati.
Pia ameeleza kuwa Serikali haina taarifa zozote kuhusu vitendo vya wizi katika Kiwanda cha Musoma Dairy.

