Na Lucy Lyatuu, Dodoma
MAMLAKA ya Rufani za Zabuni za Umma (PPAA) imesema inahakikisha wazabun wanapata haki zao zinazostahili kwa kutumia mfumo wa moduli ya kushughulikia malalamiko ya zabuni ulioanza kutumika rasmi Februari 2025.
Imesema mfumo huo unaendelea kuongeza ufanisi, uwazi na kasi ya usikilizaji wa mashauri ya wazabuni .
Katibu Mtendaji wa PPAA, James Sando amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea Chinangali, jijini Dodoma, na kuongeza kuwa katika mwaka huu wa fedha mamlaka hiyo inapokea na kushughulikia malalamiko mengi ya wazabuni yanayowasilishwa kutoka taasisi mbalimbali za umma kupitia mfumo huo.
Amesema moduli hiyo inaunganisha taasisi zote za serikali pamoja na wazabuni wote waliosajiliwa katika mfumo wa NeST, hatua inayolenga kutatua changamoto zilizokuwa zikijitokeza katika usimamizi wa malalamiko ya zabuni.
” Kabla ya kuanzishwa kwa mfumo huo, wazabuni wanalazimika kutumia muda na gharama kubwa kufuatilia malalamiko yao kwa kufika ofisini, hali inayowaathiri katika shughuli zao za biashara,” amesema.
Amesema hata hivyo, kupitia moduli hiyo, mzabuni sasa anaweza kufuatilia hatua ya shauri lake kwa njia ya mtandao na kujua kwa uwazi taasisi inayolishughulikia.
Ameongeza kuwa mfumo huo pia unaondoa changamoto ya upatikanaji wa nyaraka, kwani taarifa zote zinazohusiana na zabuni zinahifadhiwa ndani ya moduli. Hali hiyo inawezesha PPAA kupata nyaraka zinazohitajika kwa wakati, hivyo kufanya maamuzi kwa haraka, kwa ufanisi na kwa kuzingatia misingi ya haki.

