Na Safari ya Tanzania kuelekea Dira ya Maendeleo 2050
Na Lucy Ngowi
KATIKA wakati ambao Tanzania inaelekea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga uchumi wa kisasa, matumizi ya teknolojia, uhifadhi wa mazingira na ajira kwa vijana, watafiti kutoka Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), wameibuka na mradi bunifu wa ufugaji wa inzi chuma.
Mradi unaotajwa kuwa suluhisho la changamoto ya protini kwenye chakula cha mifugo pamoja na usimamizi wa taka ozo.
Mradi huo unaoongozwa na mhadhiri wa Idara ya Kemia, Dkt. Lucas Luchemba, unatumia taka ozo kuzalisha funza wenye kiwango kikubwa cha protini kwa ajili ya chakula cha kuku, samaki, nguruwe na mifugo mingine.

Kwa mujibu wa watafiti hao, Tanzania na dunia kwa ujumla zinakabiliwa na changamoto kubwa ya gharama za chakula cha mifugo kutokana na utegemezi wa vyanzo vya kawaida vya protini kama samaki na soya, ambavyo pia hutumiwa na binadamu.
“Tuliona kuna haja ya kutafuta njia mbadala ambayo itapunguza gharama za uzalishaji wa mifugo lakini wakati huohuo itoe suluhisho la mazingira,” anasema Dkt. Luchemba.
Anasema tafiti zinaonyesha funza wa inzi chuma wana kiwango cha protini kinachofikia asilimia 55 hadi 60, kiwango kilicho juu zaidi kuliko soya au samaki ambazo mara nyingi huwa kati ya asilimia 30 hadi 35.
Anasema kutokana na ubora huo, kilo moja ya funza inaweza kutoa matokeo makubwa zaidi kwenye lishe ya mifugo kuliko kiasi kikubwa cha soya, jambo linalopunguza gharama kwa wafugaji na kuongeza uzalishaji.

Mradi huo unaendana moja kwa moja na Dira ya Maendeleo 2050 kwa sababu unachangia sekta muhimu zinazotarajiwa kuendesha uchumi wa Tanzania , ikiwemo kilimo cha kisasa, viwanda, teknolojia na uchumi wa kijani.
Anasema kupitia mradi huo, taka ozo zinazochafua mazingira zinabadilishwa kuwa bidhaa zenye thamani ya kiuchumi kama chakula cha mifugo, mafuta na mbolea ya asili.
Kwamba, hatua hiyo inaunga mkono azma ya taifa ya kujenga uchumi unaotunza mazingira huku ukiongeza thamani ya rasilimali zilizopo.
Maelezo yake ni kwamba, inzi chuma ni wadudu wa kawaida waliopo kwenye mazingira yanayozunguka jamii, na wameumbwa kusaidia kusafisha mazingira kwa kula taka zinazooza.
Funza wao hubadilisha taka hizo kuwa protini na mbolea yenye virutubisho vingi.
Mbali na protini, mradi huo pia huzalisha mafuta yenye matumizi mbalimbali kwenye utengenezaji wa sabuni, vipodozi na hata tafiti za biodizeli.
Hii inaonesha namna teknolojia hiyo inaweza kuchochea viwanda vidogo na kuongeza thamani ya mazao ya ndani.
Faida nyingine kubwa ni uzalishaji wa mbolea asilia inayobaki baada ya funza kuchakata taka.
Mbolea hiyo huongeza rutuba ya udongo na kusaidia kupunguza matumizi ya kemikali kwenye kilimo, hatua inayosaidia kulinda afya ya udongo na mazingira.
Anasema katika utekelezaji wa Dira ya 2050, suala la ajira kwa vijana na elimu ya vitendo limepewa kipaumbele.

Mradi huo tayari umeanza kutoa mafunzo kwa wanafunzi wa vyuo na shule mbalimbali kuhusu namna ya kutumia sayansi na teknolojia kutatua changamoto za jamii.
“Tunaamini vijana wakipewa ujuzi huu wataona taka kama fursa ya biashara badala ya uchafu,” anasema.
Dkt. Luchemba anasema, matarajio ndani ya miaka mitatu kufikia zaidi ya vikundi 2,000 vya vijana na wajasiriamali ili kuwajengea uwezo wa kuzalisha funza, kutengeneza chakula cha mifugo na kuchakata taka ozo kwa matumizi ya kiuchumi.
Aidha, mradi huo unaonekana kuwa sehemu ya suluhisho la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kupunguza taka zinazooza kwenye madampo ambazo huzalisha gesi hatari ya ukaa.
Kwa upande wake, Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imekuwa mdau muhimu katika kukuza ubunifu huo.
Kwamba, Costech imewapatia watafiti mafunzo ya ujasiriamali wa teknolojia, usimamizi wa miradi bunifu na namna ya kubadilisha tafiti kuwa bidhaa zinazofika sokoni.
Pia imeendelea kuwapa ushauri wa kitaalamu na kuwawezesha kuanza mchakato wa usajili wa hati miliki kupitia Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) ili kulinda ubunifu wao.
Watafiti hao wanaamini kuwa kama kutakuwa na uwekezaji wa kutosha katika miundombinu, mashine na maeneo ya uzalishaji, mradi huo unaweza kuwa miongoni mwa teknolojia zitakazosaidia Tanzania kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo 2050,
Kwa kuongeza uzalishaji wa mifugo, kulinda mazingira na kufungua maelfu ya fursa za ajira kwa vijana.

